24 C
Dar es Salaam
Saturday, May 4, 2024

Contact us: [email protected]

… WAKUU WA MIKOA WAMUIGE MAKONDA

Na ELIZABETH HOMBO-DAR ES SALAAM


RAIS Dk.John Magufuli, amemwagiza Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kuwafundisha wakuu wa mikoa nchini  wamuige Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda katika utendaji wa kazi.

Aalitoa kauli hiyo  Dar es Salaam jana, wakati akifungua Mkutano Mkuu wa 33 wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) ambao uliwakutanisha mameya kutoka mikoa yote nchini.

“Makonda nimesikia unakusanya hela kwa ajili ya maendeleo, umekusanya shilingi ngapi?

Makonda alijibu kuwa ni Sh milioni 186.

Rais akaendelea: “Sasa kwa nini wakuu wa mikoa wengine hawaigi kwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam? Waziri Mkuu hebu wafundishe wakuu wa mikoa wengine waige kwa Makonda”.

Rais Magufuli pia alizungumza  vita dhidi ya dawa za kulevya akisema Makonda alipojaribu akaandamwa sana huku wengine wakisema hajasoma.

“Nchi hii ilikuwa sehemu ya dawa za kulevya. Watoto wetu tunaozaa wanatoa makamasi, watoto wa hao wanao-supply hizo dawa hawatoi makamasi.

“Sasa Makonda alipojaribu kidogo, vita ikawa kubwa… mara  hajasoma…hajafanya nini…mimi hata hajui … lakini mradi anashika dawa za kulevya huyo ni msomi mzuri.

“Kwani wenyeviti mliopo hapa wote mmesoma? Kwani halmashauri haziendi vizuri? Kwa sababu hata wasomi wenyewe wametuangusha.

“Na huo ndiyo moyo tunaotaka kuujenga kwa watanzania tuwe na uzalendo. Hivyo tumeendelea kuwashughulikia na nimeshawaambia hata huko nje ukishikwa kule sheria za kulekule zitumike… kama China wananyonga, wakunyonge huko huko.

“Kwa sababu wakiwaleta huku mimi naogopa kuwanyonga lakini ukishikwa huko ukanyongwa thank you (asante).  Sheria za kule zikatumike tena haraka haraka kwa sababu madhara yake ni makubwa kwa watanzania.

“Madawa ya kulevya tulikuwa tunayasikia mjini lakini siku hizi hadi vijijini yapo, wapo wavuta madawa. Kulikuwa kuna mtu mkubwa hapa nchini ni mfanyabiashara ametetewa sana, nikasema huyu shika peleka tukasafirisha Marekani. “Akashughulikiwe huko akimaliza kule kushughuliliwa na kule kuna adhabu ya kunyongwa.

“Ukiwagusa hawa waliokuwa wanapata fedha kwa madawa ya kulevya usitegemee kama watakupenda na mimi sihitaji wanipende lakini vijana tutakaokuwa tumewaokoa ni wengi watajibu siku moja kwa ajili ya watanzania,” alisema.

Februari 2, mwaka huu, Makonda alitaja kwa mara ya kwanza majina ya watu aliodai wanahusika na dawa za kulevya.

Tangu alipochukua uamuzi huo alianza kuandamwa huku suala la elimu na majina yake halisi likiibuka na baadhi ya wabunge wakipinga utaratibu alioutumia wa kuwataja hadharani watuhumiwa hao.

Wabunge hao pia walitaka kiongozi huyo achunguzwe kwa madai ya kupata ukwasi wa kutisha ndani kipindi kifupi.

Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima ambaye naye alitajwa na Makonda katika orodha ya watuhumiwa wa dawa za kulevya.

Alidai  jina halisi la kiongozi huyo ni Albert Bashite na jina la Paul Makonda lilipatikana baada ya kuamua kutumia cheti cha mtu mwingine baada ya kushindwa mtihani wa kidato cha nne.

Gwajima alidai kuwa majina halisi ya kiongozi huyo ni Daudi Albert Bashite na kwamba jina la Paul Makonda lilipatikana baada ya kuamua kutumia cheti cha mtu mwingine baada ya kushindwa mtihani wa kidato cha nne.

Si Makonda wala mamlaka yake ambayo imepata kulizungumza kwa undani suala hilo na yeye mwenyewe amekuwa akipuuza taarifa hizo kila anapoulizwa na vyombo vya habari.

Tayari Meya wa Ubungo, Bonifance Jacob, amewasilisha mashitaka dhidi ya Makonda kwa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, akitaka achukuliwe hatua za  nidhamu kwa kukiuka maadili ya utumishi wa umma na hivyo kukosa sifa ya kuwa kiongozi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles