24.8 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

UHURU WA KUJIELEZA: HAKI INAYOLINDWA KIKATIBA INGAWA BADO INAMINYWA

Na NORA DAMIAN


WIKI mbili zilizopita nilitumiwa ujumbe wa WhatsApp ambao ulikuwa umejaa mafumbo mengi na ilinilichukua muda kidogo kuweza kuyang’amua kwani yalikuwa ni magumu.

Baada ya kutafakari na kuyang’amua nilijikuta nikiwa nacheka mwenyewe; nilijiuliza maswali mengi lakini kubwa nililoliona ni kwamba watu sasa wana hofu ya kujieleza. 

Ndio maana wanatumia mbinu mbalimbali katika mazungumzo yao kama vile kwenye simu, mitandao ya kijamii kwa kuepuka kutaja watu kwa majina ama nyadhifa zao.

Mathalani katika mitandao mbalimbali ya kijamii watu wamekuwa wakiijadili serikali na viongozi kadhaa akiwamo rais huku wakitumia mafumbo na a.k.a nyingi.

Si ajabu sasa ukiingia katika mitandao ya kijamii na kukutana na mijadala mingi inayojadiliwa kimafumbo na kadiri siku zinavyozidi kwenda ndivyo staili ya mijadala nayo inabadilika.

Mathalani kama kiongozi fulani alikuwa akiitwa kwa a.k.a fulani na ikaonekana imekuwa gumzo basi hutafutwa a.k.a nyingine.  

Tumefika huko kutokana na hofu iliyoanza kujengeka kwamba taarifa mbalimbali hivi sasa zinafuatiliwa huku mamlaka zikimulika watumiaji wanaodaiwa kuandika maneno hasa yale yenye mlengo wa kukosoa.

Mara kadhaa ukosoaji umetafsiriwa kwa namna nyingi ikiwamo kuchochea lakini kuna ukweli kupitia ukosoaji husika unaweza kujifunza ama kujua kitu kinachoendelea juu ya jambo fulani.

Kwa ujumla haki ya uhuru wa kujieleza inahusisha haki ya kutafuta, kupokea na kusambaza taarifa na mawazo.

Haki hii ina uwanja mpana; kwa kuangalia dhana ya kusambaza taarifa na mawazo, haki hii inahusisha haki ya mtu kujieleza ana kwa ana, kwa maandishi, kwa kutumia njia zingine za mawasiliano pamoja na njia za kielektroniki.

Haki ya uhuru wa kujieleza inahusisha pia haki ya kutafuta na kupokea taarifa kutoka kwa wengine, pamoja na haki ya kupata na kusoma magazeti, kusikiliza matangazo, kutumia mtandao wa intaneti na kushiriki kwenye mijadala ya umma au binafsi.

Haki ya uhuru wa kujieleza inalindwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, chini ya ibara ya 18. Haki hii pia inalindwa na mikataba mbalimbali ya kimataifa kama vile Tamko la Kimataifa la Haki za Binadamu katika ibara ya 19, Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kisiasa na Kiraia katika ibara ya 19 na Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu katika ibara ya 9.

Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kisiasa na Kiraia umeorodhesha masharti kadhaa ambayo yanapaswa kufuatwa wakati wa kutafuta, kupokea na kusambaza taarifa.

Hii ina maana kuwa haki ya uhuru wa kujieleza inaweza kuwekewa mipaka ya utekelezwaji wake na dola, isipokuwa tu mipaka hiyo lazima iwe inawekwa kwa mujibu wa sheria au kanuni, isizidi faida ya masilahi iliyokusudiwa.

Taarifa ya Haki za Binadamu ya mwaka 2015 iliyotolewa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), inaonyesha licha ya kuwa na ulinzi wa kikatiba bado kuna sheria nyingi zinazobana uhuru wa kujieleza.

Kutokana na hali hiyo kituo hicho kimeanzisha Kampeni ya Kulinda Uhuru wa Kujieleza na Kukusanyika ambayo inalenga kuibua mjadala juu ya haki za kiraia na haki za kisiasa nchini.

Kampeni hiyo iliyobeba kaulimbiu ya ‘Bila uhuru wa kujieleza na kukusanyika hatuwezi kuendelea’ ilizinduliwa wiki iliyopita jijini Dar es Salaam na inatarajiwa kuhitimishwa Novemba mwaka huu.

Kampeni hiyo imeandaliwa na LHRC kupitia mradi wa Uhakiki kwa kushirikiana na wadau washirika ambao ni Jukwaa la Wahariri (TEF), Baraza la Habari (MCT), Policy Forum, Twaweza, Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD), Shirika la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Afrika (WiLDAF) na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.

Wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo, wadau washirika walipaza sauti zao na kutaka utungaji wa sheria zinazoathiri haki ya uhuru wa kujieleza uangaliwe upya kwa kuhusisha wadau mbalimbali.

Kwamba sheria zinatakiwa kuweka bayana haki, jukumu na wajibu wa ulinzi wa haki ya uhuru wa kujieleza kwa serikali na raia.

Mkurugenzi wa Utetezi na Maboresho wa LHRC, Ana Henga, anasema uhuru wa kujieleza ni muhimu kwani unaweza kulitoa taifa kutoka hapa lilipo na kuliwezesha kusonga mbele.

 “Watu wengi wanaogopa kujieleza, vyombo vya habari vinafungiwa kwa ujumla hali si nzuri, uhuru wa kujieleza na kukusanyika uko katika hatihati,” anasema Henga.

MCT

MCT ni mojawapo wa wadau washirika katika kampeni hiyo, Ofisa Mwandamizi kutoka MCT, Paul Malimbo, anazitaja sheria kinzani kuwa ni Sheria ya Takwimu ya mwaka 2015, Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari ya mwaka 2016 na Sheria ya Makosa ya Mtandaoni ya mwaka 2015 na kupendekeza zifanyiwe marekebisho kuendana na katiba na mikataba ya kimataifa na kikanda ambayo taifa limeridhia.

JUKWAA LA WAHARIRI

Jukwaa la Wahariri Nchini nao pia ni wadau washirika katika kampeni hiyo ambapo Mwenyekiti wa TEF, Theophil Makunga, anasema wanashiriki ili kuwafanya watu wajieleze wapate habari za kuandika.

“Uhuru wa kujieleza na kukusanyika ni muhimu sana kwa waandishi wa habari kwani huwarahishia kupata habari, kama mtu ajielezi mwandishi huwezi kupata habari mfano unaenda kwa source (mtoa habari) halafu kafunga mdomo, kwahiyo chanzo cha kazi yetu sisi ni lazima mtu ajieleze, “anasema Makunga.

TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA

Ofisa wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Costantine Luguli, anasema eneo la haki za binadamu bado lina utata mwingi ambao pia unachangiwa na watu kutokuwa na ufahamu wa kutosha.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles