MWANAMUZIKI aliyepitia changamoto za matumizi ya dawa za kulevya, Rehema Chalamila ‘Ray C’, mwishoni mwa wiki anatarajiwa kufanya onyesho nchini Kenya.
Onyesho hilo la kumrudisha mwanadada huyo aliyewahi kujizolea umaarufu mkubwa kutokana na uwezo wake wa kukata kiuno na kuimba litafanyika katika mji wa Malindi.
Umbo na uwezo wake wa kunengua kwa madoido na sauti nzuri aliyokuwa nayo ndivyo vilivyompa umaarufu kwa idadi kubwa ya wapenda burudani nchini Kenya, Uganda na Tanzania.
Lakini hata hivyo, muda aliotumia katika nyumba ya kutunzia wanaotumia dawa za kulevya ulibadilisha umbo lake ambalo wengi wanataka kuona namna anavyoweza kulitumia wakati atakapokuwa akiimba kama atakuwa kama alivyokuwa zamani.