23.3 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Walanguzi wa mbolea nchini kusakwa

dk-charles-tizebaNa JONAS MUSHI -DAR ES SALAAM

SERIKALI imesema inawasaka wafanyabiashara wa mbolea wanaopandisha bei kwa wakulima licha ya bei na gharama za  uzalishaji wa bidhaa hiyo kushuka katika masoko ya nje.

Hayo yalisemwa jana jijini Dar es Salaam na Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Dk. Charles Tizeba, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kufungua mkutano wa jumuiya ya wazalishaji mbolea duniani ulioandaliwa na Kampuni ya Masoko ya Mbolea Duniani (CRU) kwa ushirikiano na Ushirika wa Wafanyabiashara wa Mbolea Barani Afrika (AFAP) .

Alisema bei kubwa ya mbolea imekuwa kikwazo katika kilimo suala linalosababisha wakulima wengi kutumia mbolea kidogo au kutotumia kabisa na kusababisha uzalishaji mdogo.

“Wakati wa kanuni za kilimo bora zinataka hekta moja kutumia mbolea kilo 50 Tanzania bado tupo kwenye wastani wa kilo 19.3 kwa hekta moja na sababu kubwa ni bei kubwa ya mbolea ambayo wakulima wengi wanashindwa kuimudu.

“Mwaka jana tani moja ya mbolea ya MPK iliyotolewa bandarini ilikuwa dola za Marekani 310 lakini mkulima wa kule Tabora aliuzwa tani hiyo kwa dola 1050.

“Hapa tunaona kuna tatizo hapo katikati kuna watu wanafanya mbinu ili kutengeneza faida isiyo halali na tumeanza kuchungulia kuona ni nani ili tuweze kuwaondoa,” alisema Dk Tizeba.

Alisema katika kuhakikisha bei ya mbolea inashuka Serikali imepanga kuanza kuagiza mbolea kwa pamoja kuanzia mwakani pamoja na kupunguza utitiri wa kodi katika bidhaa hiyo.

Aidha aliwaondoa hofu wakulima na kuwahakikishia kuwa katika msimu wa mwaka ujao mbolea itashuka bei kwa asilimia 25 hadi 30 ambayo itachangiwa na kushuka kwa gharama za usafiri kwa asilimia 40 kutokana na kutumia treni badala ya malori.

Awali akifungua mkutano huo Dk. Tizeba alitoa wito kwa sekta binafsi kuwekeza katika kuanziasha viwanda vya mbolea nchi huku akiwahjakikishia upatikanaji wa masoko na mali ghafi ikiwemo gesi asilia.

Akizungumzia lengo la mkutano huo Ofisa Mtendaji Mkuu wa Matukio wa CRU , Nicola Coslett, alisema umelenga kumulika mchango wa wazalishaji mbolea katika kuchochea kilimo cha biashara na namna bara la Afrika linavyoweza kushirikiana na washirika wa kimataifa kuinua sekta ya kilimo.

Kwa upande wake Makamu wa Rais wa AFAP , Richard Mkandawire, alisema mbolea ni nguzo muhimu kwa katika uzalishaji wa chakula na uwepo wa viwanda madhubuti vya mbolea kutachochea ongezeko la bidhaa za kilimo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles