24 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

TUSIPOJIPANGA AFCON 2019 ITAKUWA NDOTO

Na ADAM MKWEPU-DAR ES SALAAM


taifa-starsHIVI karibuni Shirikisho la Soka barani Afrika (CAF), limetoa droo ya makundi ya kufuzu fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (Afcon) mwaka 2019 inayotarajiwa kuchezwa nchini Cameroon.

Taifa Stars imepangwa Kundi L pamoja na timu za Uganda, Cape Verde na Lesotho katika droo iliyopangwa wiki iliyopita mjini Libvreville, Gabon, zinapofanyika fainali za mwaka huu.

Majirani zetu Kenya pia wataanzia hatua ya makundi wakiwa wamepangwa Kundi F pamoja na Ghana, Ethiopia na Serra Leone, wakati Rwanda ipo Kundi H pamoja na Ivory Coast, Guinea na Afrika ya Kati (CAR).

Wenyeji wa michuano hiyo timu ya Cameroon ambayo imefuzu moja kwa moja imepangwa Kundi B pamoja na timu za Morocco, Malawi na mshindi kati ya Comoro na Mauritius.

Kwa haraka haraka, katika Kundi L linaonekana kuwa ni upenyo kwa timu ya soka ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ kufanya vizuri zaidi kwani ni Uganda pekee ndio ambao huenda wakaibabaisha.

Uganda kwa sasa ndio vinara wa soka ukanda wa Afrika Mashariki hivyo haitakuwa kazi rahisi kupata ushindi kutoka kwao.

Bila maandalizi ya kutosha ni wazi kundi hilo bado litakuwa gumu kwa Stars kwani kila upande unajiandaa vema katika michuano hii.

Hakuna kundi jepesi au gumu ni vile ambavyo timu husika itajiandaa kuwavaa wapinzani wake na kuonesha dhamira ya kufanya mapinduzi katika soka.

Kwa kipindi kirefu tumekuwa na hamu ya kutaka kushiriki michuano hiyo mikubwa Afrika yenye mvuto wa aina yake.

Tanzania imeshiriki mara moja tu Afcon, mwaka 1980 iliyokuwa ikichezwa nchini Nigeria tena wakati huo bado zikiitwa Fainali za Kombe za Mataifa Huru ya Afrika.

Na mwaka huo, Taifa Stars iliyopangwa Kundi A pamoja na wenyeji Super Eagles, Mafarao wa Misri na Tembo wa Ivory Coast, ilishika mkia baada ya kufungwa mechi mbili 3-0 na Nigeria, 2-1 na Misri na 1-1 na Ivory Coast.

Michuano hiyo itaanzia kwa hatua ya mchujo, raundi ya awali itakayohusisha timu za Comoros, Djibouti, Madagascar, Mauritius, Sao Tome E Principe na Sudan Kusini.

Timu zitakazofuzu hapo zitaingia moja kwa moja kwenye makundi A, B na C kukamilisha idadi ya timu nne nne. Kundi A lina timu za Senegal, Equatorial Guinea na Sudan, B kuna wenyeji Cameroon, Morocco na Malawi na C kuna Mali, Gabon n Burundi.

Stars ambayo ipo chini ya kocha wa muda, Salum Mayanga, itakuwa na wakati mgumu ikiwa bado itashindwa kuchanga karata zake vizuri.

Siasa zikiwekwa kando Stars wanaweza kurejea kwenye Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2019 kwa kishindo na kuweza kufanikiwa kufika mbali lakini tofauti na hapo hali itaendelea kuwa ile ile ambayo imezoeleka kila kukicha.

Kwani ni bahati ya kipekee kupangwa katika kundi jepesi ambalo kama maandalizi yatakuwa mazuri Stars itafanikiwa kufuzu.

Mara kadhaa matokeo ya siasa katika soka yameonekana kuyumbisha kupiga hatua za maendeleo ikiwa pamoja na kushiriki katika michuano mikubwa Afrika.

Kwa sasa Stars ili ifanikiwe kufuzu kucheza michuano hiyo inatakiwa kufanya maamuzi magumu mapema kuhakikisha inajipanga vema na kupata mafanikio katika michuano hiyo.

Suala la migogoro isiyokuwa na maana pamoja na malumbano ya masilahi binafsi hayana budi kuachwa ili kuongeza nguvu ya pamoja iwapo tunataka kufanya vizuri katika michuano hiyo.

Aidha, hatua ya mchujo itachezwa kati ya Machi 20 na 28 wakati mechi za kwanza za makundi zitaanza Juni 5 na 13, mwaka huu za pili Machi 19 na 27, mwaka 2018, za tatu Septemba 3 na 11, mwaka 2018 za nne Oktoba 8 na 16, mwaka 2018 na za tano Novemba 5 na 13, mwaka 2018.

Mshindi wa kila kundi atafuzu moja kwa moja Afcon 2019, wakati timu nyingine tatu zitakazomaliza nafasi ya pili na wastani mzuri zaidi ya nyingine zitafuzu kama washindi wa pili bora.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles