24.8 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Sudan yahitaji msaada kujenga upya uchumi

KHARTOUM, SUDAN

SUDAN inahitaji msaada wa dola za Marekani bilioni 8 katika kipindi cha miaka miwili ijayo ili iweze kujinasua na gharama za kuagiza bidhaa za nje pamoja na kuisaidia kuujenga upya uchumi wake uliovurugika baada ya miezi kadhaa ya vurugu za kisiasa.

Hayo ni kwa mujibu wa Waziri Mkuu mpya wa taifa hilo, Abdallah Hamdok, ambaye amekula kiapo chake siku chache zilizopita.

Kiongozi huyo ambaye ataongoza Serikali ya mpito katika kipindi cha miaka mitatu ijayo, alisema kiasi kingine cha akiba ya fedha za kigeni cha dola bilioni 2 kitahitajika ili kudhibiti kuporomoka kwa thamani ya sarafu ya nchi hiyo.

Mchumi Hamdok mwenye umri wa miaka 61, ambaye amewahi kufanya kazi katika kamisheni ya uchumi ya Umoja wa Mataifa kwa Afrika, alisema ameanza kufanya mazungumzo na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) na Benki ya Dunia, yenye lengo la kufanya marekebisho ya deni la Sudan na kuyashawishi mataifa rafiki na vyombo vingine vya fedha kuhusu msaada huo.

Katika mahojiano yake na Reuters, Hamdok alisema katika kipindi cha miaka miwili ijayo, Sudan italazimika kulipa madeni na kufanya juhudi kubwa za kufufua uchumi wake kwani imedhoofishwa sana na mgogoro wa miezi kadhaa sasa wa kisiasa.

Alisema Sudan hivi sasa inahitaji msaada wa kigeni wa zaidi ya dola bilioni nane kuweza kukabiliana na changamoto zake nyingi, hasa za kiuchumi.

Aliongeza kuwa mazungumzo baina yake na Mfuko wa Kimataifa wa Fedha na Benki ya Dunia yameshaanza kama juhudi za kuyashawishi mashirika hayo muhimu ya kifedha ya kimataifa kuipatia tena mikopo Sudan.

Jumatano iliyopita, Hamdok alikula kiapo cha kuwa Waziri Mkuu wa Serikali ya mpito ya Sudan.

Baraza la Mpito la Kijeshi la Sudan limekuwa likitawala nchini humo tangu Aprili 11, mwaka huu baada ya kupinduliwa Jenerali Omar al Bashir.

Mara kwa mara baraza hilo lilikuwa likituhumiwa kukwamisha mambo ili kuzuia utawala wa kiraia nchini humo, lakini kusimama imara wananchi katika maandamano kumelilazimisha baraza hilo la kijeshi linaloungwa mkono na Saudi Arabia, Imarati na Misri lisalimu amri na kuruhusu kushirikishwa kikamilifu wananchi katika utawala.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles