24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

SHISHA YATAJWA CHANZO CHA MAPATO YA SERIKALI

LEONARD MANG’OHA-DAR ES SALAAM


 

shishaLICHA ya kupigwa vita na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, imebainika kwamba shisha ni chanzo cha mapato ya Serikali.

Utafiti uliofanywa na MTANZANIA na kuthibitishwa na baadhi ya wabunge, shisha inatambuliwa na sheria ya kodi ya mwaka 2016 iliyopitishwa na Bunge Juni mwaka huu kama chanzo cha mapato.

Katika bajeti kuu ya Serikali iliyosomwa bungeni na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango Juni mwaka huu shisha ni mojawapo ya vyanzo hivyo ikiwa katika kundi la mazao yatokanayo na tumbaku.

Sehemu ya hotuba hiyo inaelekeza kufanyika kwa marekebisho ya viwango maalumu vya kodi (specific duty rates) kwenye ushuru wa sigara zisizo na kichungi zinazotengenezwa kutokana na tumbaku inayozalishwa hapa nchini kwa kiwango cha angalau asilimia 75, kutoka shilingi 11,289 hadi shilingi 11,854 kwa kila sigara elfu moja.

Aidha ushuru wa “cigar” pamoja na sigara nyingine za kutoka nje, zilielezwa kuwa unabaki kuwa asilimia 30 huku tumbaku ambayo iko tayari kutengeneza sigara (cut filler) ikipanda kutoka shilingi 24,388 hadi shilingi 25,608 kwa kilo.

Aidha baadhi ya wabunge wa Kamati ya Bunge ya Bajeti waliiambia MTANZANIA kuwa kilevi hicho (shisha) ni miongoni mwa vyanzo halisi vya mapato ya Serikali na kwamba kuipiga marufuku ni kukataa mapato halali ambayo yamewekwa kisheria.

Mbunge wa Momba, David Silinde (Chadema) alisema katazo lolote kuhusu bidhaa hiyo ya shisha ni batili kisheria.

Silinde ambaye pia ni mjumbe wa Kamati ya Bunge ya Bajeti alisema katika vyanzo vya mapato kwa mujibu wa hotuba ya bajeti ya Serikali iliyosomwa mwaka huu na Dk. Mpango, shisha inaangukia katika kundi la sigara nyinginezo na bidhaa hizo zinatozwa asilimia 30 ya kodi.

“Hivi nyinyi hamshangai, statement (taarifa) inatoka kwa mtu mmoja ambaye kimsingi anatafuta chiep politics (umaarufu) asiokuwa nao.

“Shisha sio bangi, duniani kote watu wanatumia shisha kama kiburudisho chao, ni kama sigara ambavyo inatajwa kuwa na madhara lakini watu wanatumia. Ni suala la mtu binafsi kutumia au kutotumia.

“Kama ni madhara ya kiafya wizara yenye dhamana na afya wajitokeze watoe tamko ambalo halitapingana na taasisi nyingine zikiwamo za kimataifa” alisema Silinde.

Mjumbe mwingine wa kamati hiyo, Mbunge wa Babati,  Vrajilal Jituson (CCM) yeye alikiri kuwa kilevi hicho ni miongoni mwa vyanzo vya mapato vya serikali na imeorodheshwa katika Sheria ya fedha (Finance bill Act) ya mwaka 2016.

Hata hivyo alisema licha ya kuwapo kwa sheria ya kodi inayoruhusu kuingizwa nchini kwa bidhaa hiyo si jambo la ajabu kupiga marufuku bidhaa hiyo.

“Ninavyofahamu mimi shisha haina ubaya ila nadhani kinachofanyika Dar es Salaam wauzaji wanachanganya na dawa za kulevya, bangi, tumbaku na vitu vingine inageuka kuwa kilevi kisichofaa.

“Utumiaji wa shisha ni utamaduni wa kiarabu ambapo watu wote wanawake kwa wanaume walikuwa wakivuta kama kiburudisho na kusema kuwa shisha ni kama ‘pool table’ ambao ni mchezo kama michezo mingine lakini umegeuzwa na kuwa kamali hivyo kuharibu maana halisi ya mchezo huo” alisema Jituson.

 

Waziri kivuli wa Fedha

Waziri Kivuli wa Fedha, Halima Mdee (Chadema) yeye alisema suala la shisha ni matokeo ya watendaji wa serikali kufanyakazi kwa matukio.

Mdee ambaye pia ni Mbunge wa Kawe (Chadema) alisema shisha ni chanzo halisi cha mapato kwa mujibu wa sheria ya fedha iliyopitishwa na Bunge Juni mwaka huu.

Alisema marufuku yoyote dhidi ya bidhaa hiyo  ni suala ambalo halitekelezeki kwa sababu limefungwa na sheria na kwamba wale wanaolizungumza kisiasa wapuuzwe.

“Tatizo ninaloliona hapa ni serikali kufanyakazi kwa matukio, lakini pia hawa wenzetu hawasomi vitu, hiyo sheria ya shisha waliipitisha wenyewe sisi tukiwa nje katika Bunge la bajeti mwaka huu.

“Siku zote sisi tukiwa mle ndani huwa tunapitia na kusoma nyaraka kwa umakini, leo sheria waliyoitunga wao hawaikumbuki” alisema Mdee.

Kilevi hicho kwa mara ya kwanza kilipigwa marufuku na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwa katika hafla ya kufuturisha waumini wa dini ya Kiislamu wa madhehebu ya Shia Juni mwaka huu.

Waziri Mkuu alidai kuwa shisha ni kilevi ambacho huchanganywa na vitu vingine vikiwamo viroba na pombe nyingine haramu.

Baadaye Mkuu wa Mkoa, Paul Makonda aliendelea kushikia bango suala hilo ambapo hivi karibuni alikwenda mbali zaidi kwa kuwatuhumu Kamanda wa Polisi, Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Simon Sirro pamoja na Kamanda wa Polisi wa Kinondoni kuwa huenda wanapokea rushwa kutoka kwa wauza shisha.

Katika salamu zake wakati wa uzinduzi wa Mradi wa Uboreshaji wa Miundombinu ya Umeme katika Jiji la Dar es Salaam, Makonda alimweleza waziri mkuu kuwa wafanyabiashara wa shisha walikwenda ofisini kwake na kumwahidi kumpa Sh milioni 5 kila mwezi ili asiwasumbue.

“Shisha imerudi katika mkoa huu lakini nimeona kama Sirro ana kigugumizi… sijajua kama hizi tano tano zimepita kwake na pia RPC wa Kinondoni nimemuona hapa, sijui kwa nini hawa wana kigugumizi, sijui kama hizi tano tano zimepita kwao,” alisema Makonda.

Katika majibu yake, Waziri Mkuu, Majaliwa alisema atamwajibisha Makonda iwapo hatasimamia ipasavyo kukomesha matumizi ya dawa za kulevya, aina ya shisha.

Wizara ya Fedha

Akizungumzia suala hilo, Kaimu Msemaji wa Wizara ya Fedha na Mipango, Benny Mwaipaja alisema kuwa lengo la serikali yoyote ni kulinda afya za wananchi wake kadiri iwezekanavyo na ikiwa itabainika kuna madhara yanayotokana na matumizi ya shisha basi uamuzi huo utakuwa si sahihi.

“Kama wafanyabiashara wa shisha Dar es Salaam wamekiuka masharti na vigezo vya kuendesha biashara hiyo uamuzi wa mkuu wa mkoa ni sahihi” alisema Mwaipaja.

Aidha Mwaipaja alisema wizara itaendelea kulifuatilia suala hilo kufahamu kama kuna madhara ya kiafya yanayotokana na matumizi ya shisha pamoja na kuangalia kama uamuzi wa kuzuia kuuzwa kwa shisha pia ni sahihi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles