Na Brighiter Masaki, Mtanzania Digital
MBUNIFU wa mavazi nchini, Ally Remtullah, ameiomba Serikali kupunguza bei za malighafi za kutengenezea nguo ili watu waendelee kupenda vya nyumbani zaidi.
Akizungumza na Mtanzania Digital, Remtullah amesema anawapongeza wadau mbalimbali wanaoendelea kutoa ushirikiano na kununua kazi za wabunifu hao hususani viongozi,wasanii pamoja na wanamichezo.
“Sheria ngowi amebuni jezi ya timu ya Yanga ni kitu kizuri kwa namna moja au nyingine inaonyesha wazi kuwa wabunifu tunaendelea kupewa nafasi katika jamii lakini ingependeza zaidi jezi hiyo ingetengenezwa hapa hapa nchini ila kutokana na kuwepo kwa shida ya baadhi ya malighafi imelazimika jezi hiyo kutengenezwa nje ya nchi,” amesema.
Amesema kwa sasa amejikita zaidi kusaidia wabunifu chipukizi kupitia darasa lake alilolipa jina la “Remtulah 010 ” ikijumuisha wabunifu wakubwa pamoja na watoto.
“Ni darasa ambalo linafanyika kwa miezi mitatu yenye vitendo na ninawapa nafasi kuwaandalia jukwaa la kuonyesha kazi ama vitu ambavyo wamebunia kuanzia watoto pamoja na wakubwa na katika darasa hilo watoto ni bure kabisa hakuna malipo,” amesema
Amesema kupitia darasa hilo linampa nafasi mkufunzi kujitangaza kibiashara.