24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Nchi za Afrika hatarini kusambaa corona

GENEVA, SWITZERLAND

IDADI kubwa ya nchi za Afrika ziko katika hatari kubwa ya kuingiza virusi vya Corona kutokana na mwingiliano mkubwa wa usafiri wa anga kati ya pande hizo.

Hatari hiyo inatokana na kushamiri kwa biashara kati ya China ya Afrika baada ya uwekezaji mkubwa uliofanywa na taifa hilo barani humo katika kipindi cha muongo mmoja na kuimarisha uhusiano wake wa kiuchumi na Afrika, jambo lililoongeza safari za ndege kati ya pande hizo kwa zaidi ya asilimia 600 katika kipindi hicho.

Hadi sasa bara hilo lina idadi ndogo ya visa vya ugonjwa huo vilivyothibitishwa lakini wataalamu wa afya ya wamekuwa na wasiwasi juu ya uwezekano wa kuenea zaidi kwa ugonjwa huo barani za Afrika kunatokana na mifumo dhaifu ya afya  kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO).

Taarifa ya WHO inaeleza kuwa ikiwa virusi hivyo vitaingia katika nchi inayokabiliwa na magonjwa mwengine kama vile Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo inayokabiliwa na ugonjwa hatari wa Ebola itakuwa vigumu zaidi kuvidhibiti virusi hivyo.

Taarifa hiyo inaeleza kuwa hadi mwanzoni mwa mwezi uliopita ni nchi mbili tu za Afrika (Senegal na Afrika Kusini) ndizo zilizokuwa na uwezo wa maabara wa kubaini virusi vipywa vya corona.

Mataifa ya Nigeria na Ethiopia yako katika hatari ndogo ya kuingiza virusi hivyo lakini yanaweza kuwa katika hatari zaidi kutokana na mazingira yake ya kijamii na kisiasa. 
Nchi zote mbili pia zina idadi kubwa ya watu ambayo huongeza hatari ya kusambaa haraka kwa virusi hivyo ikiwa vitafanikiwa kuingia katika mataifa hayo.
Mataifa ya Moroko, Sudan, Angola, Tanzania, Ghana, na Kenya yako katika kiwango cha wastani cha kuenea ugonjwa huo.
Wakati huo huo Korea Kusini imeripoti ongezeko kubwa la visa vipya vya maambuziki ya virusi hivyo wakati Shirika la Afya Duniani (WHO) likiutaja kuwa katika kiwango cha juu cha tishio la virusi vya Corona. 
Ongezeko hilo la visa vipya vya maambukizi ya virusi hivyo hatari zaidi duniani kwa siku za karibuni linalifanya taifa hilo kuwa nchi ya pili kwa kiwango kikubwa cha maambukizi nje ya China ambako ugonjwa huo ulianzia mapema Januari mwaka huu.
Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa jana zilionesha kuwa taifa la Bara la Asia lina jumla ya visa 3,150 vya Corona baada ya watu wengine wapya 813 kugundulika kuambukizwa virusi hivyo vinavyoendelea kusambaa kote duniani tangu vilipogunduliwa mjini Wuhan.
Mlipuko wa ugonjwa huo tayari umeanza kuleta athari za kiuchumi katika baadhi ya mataifa kwa kuathiri masoko ya mitaji katika viwango ambavyo havijawahi kushuhudiwa tangu wakati wa mdororo wa uchumi wa mwaka 2008.
Hadi sasa zaidi ya watu 2,900 wamefariki kutokana na virusi hivyo huku wengine 85,000 wakiambukuzwa duniani kote tangu vilipobainika huko Wuhan uliopo katikati ya China.

Aidha taarifa iliyochapishwa na Shirika la habari la Uingereza inaeleza kuwa utafiti uliofanya na Chuo cha Imperial College inaonesha kuwa watu tisa kati ya 1,000 walioambukizwa virusi hivyo huenda wakafariki dunia, japo hilo litategemea na mambo mbalimbali ikiwamo umri, jinsia na hali ya kiafya na mfumo wa afya ya mtu husika.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa hata jinsi ya kupata idadi kamili ya visa vya ugonjwa huo bado ni mtihani kutokana na kwa sababu watu hawaendi kwa daktari wakiwa na dalili ambazo bado hazijajitokeza vizuri.

Ilieleza kuwa idadi tofauti ya vifo vinavyoripotiwa kote duniani huenda ni kwa sababu nchi mbalimbali ama zina uwezo mzuri au bado hazina uwezo wa kubaini mapema dalili za virusi hivyo.

Utafiti huo unaonesha kuwa pia inachukua muda kabla ya maambukizi kusababisha kifo au mgonjwa kupona. Utafiti huo pia umeyataja makundi ya watu walio katika hatari ya kufa ikiwa wataambukizwa ugonjwa huo ni pamoja na wazee, wagonjwa na wanaume.

Taarifa hiyo iliongeza kuwa katika utafiti wa kwanza mkubwa uliohusisha visa zaidi ya 44,000 kutoka China, idadi ya watu waliokufa kwa ugonjwa huo ilikuwa mara 10 zaidi kwa wazee ikilinganishwa na watu wenye umri wa makamo.

Ilifafanua kuwa idadi ya watu waliokuwa na umri wa chini ya miaka 30 kufariki kwa kuambukizwa ugonjwa huo ambapo ni vifo vinane pekee ya watu walio katika kundi hilo kati ya visa 4,500 vilivyoripotiwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles