23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

MV NYERERE YASIMAMISHA HUDUMA KISIWANI UKARA

Na MASYENENE DAMIAN


KIVUKO cha MV Nyerere kinachofanya safari zake ndani ya Ziwa Victoria kati ya Bugorola-Ukara wilayani Ukerewe,   kimesimamisha huduma zake kwa zaidi ya wiki moja baada ya injini yake kupata hitilafu.

Kwa sasa boti ndogo ya MV Ukara ndiyo inayotoa huduma ya usafiri kwa wananchi huku  ikidaiwa kuzimika safarini mara kwa mara na kuhatarisha maisha ya watumiaji.

Kwa sababu hiyo hulazimika kuvutwa na kusindikizwa na boti ndogo ya usalama   inapofanya safari zake.

Kutokana na hali hiyo baadhi ya wananchi wamelazimika kutumia usafiri wa mitumbwi ya injini kufika na kutoka kisiwani Ukara kutokana na kutokuwa na imani na kivuko hicho.

Mmoja wa wasafiri, Yusuph Nzungu ambaye ni mwalimu kisiwani Ukara, alisema mara nyingi anapata safari za kwenda  Nansio   kuhudhuria semina zinazoandaliwa na halamashauri ya wilaya hiyo.

Alisema  kutokuwapo  usafiri wa uhakika kunaleta usumbufu katika kazi yake.

“Baada ya kivuko (MV Nyerere) kuharibika hivi sasa  tunalazimika kutumia boti ndogo ambazo nazo siyo za kuaminika hasa kipindi hiki cha mvua.

“Kwa hiyo tunapata usumbufu  kwa sababu boti kubwa ya Mv Nyerere imekuwa ikipata itilafu mara kwa mara inabidi waifanyie ukarabati mkubwa kuondoa kero hii,” alisema.

  Meneja wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) Mwanza, Ferdinand Mishamo, alisema kivuko cha MV Nyerere kimesimamisha huduma zake baada ya injini moja kuharibika hivyo kulazimika kuagiza injini ya akiba.

“MV Nyerere imesimama baada ya injini yake moja kuharibika tumepeleka injini ya akiba na kazi ya kubadilisha inaendelea na tunategemea kivuko kitaanza kazi baada ya siku siku mbili hivi, kwa sasa kivuko cha MV Ukara kinaendelea kutoa huduma,” alisema.

Kisiwa cha ukara ni miongoni mwa visiwa 38 wilayani ukerewe ambavyo huunganishwa kwa usafiri wa majini hivyo kuendelea kuwapo usafiri wa kusuasua kunarudisha nyuma maendeleo na shughuli za uchumi za wananchi wa visiwa hivyo.

Kivuko cha MV Nyerere kilizinduliwa mwaka 2005 na aliyekuwa Rais wa awamu ya tatu   Benjamin Mkapa kikiwa ni kivuko kikubwa ili kutatua adha ya usafiri iliyokuwapo kwa wananchi wa   Ukara.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles