Na ASHA BANI-DAR ES SALAAM
SHEIKH Mkuu, Mufti Abubakar Bin Zuber akemea baadhi ya waumini wa Kiislamu wanaotoa mawaidha ya kuwakashifu wanawake.
Mufti huyo alisema kwa kufanya hivyo ni dhahiri kuna mmonyoko mkubwa wa maadili katika uwasilishaji wa mawaidha hayo.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, kuhusu mwenendo wa utoaji wa mawaidha unaofanywa na masheikh, maimamu na walimu wa madrasa, alisema kuwa baadhi ya waumini hao wanatumia lugha za kuwadhalilisha akina mama maumbile yao.
“Si jambo jema kwa waumini wa dini ya Kiislamu kutumia lugha zisizofaa kwenye mawaidha na kudhalilisha watu hasa kwa kina mama ambao wanatajwa hadi maumbile yao jambo ambalo ni kinyume na taratibu zetu za dini.
“Mawaidha yanayotolewa na baadhi ya waumini hao pia hayana lugha ya stahakwa kuwa hayapo katika maelekezo Mtume Muhammad (S.A.W),” alisema Mufti Zubeir
Kutokana na hali hiyo alisema kuwa mawaidha yanayotakiwa ni yale yenye staha ambayo yanamshawishi anayesikiliza na kumfanya afuate mambo mema hata aliyekua si Muislamu aweze kuvutikwa nayo.
Alisema kwa wanaotumia mfumo wa kukashifu wanaharibu taswira nzuri ya dini ya kiislamu hivyo aliwataka masheikh na wanazuoni kushirikiana katika kikemea mtu yeyote anayeonekana kufanya hibyo.
“Tumeona na kusikia baadhi ya waumini wakitumia lugha ambazo zinatumia lugha za kuwadhalilisha na kuwafanya wanaonekana wananyanyasika wakati wanahitaji la kupata mawaidha yenye magunzo,”alisema
Pia alisema anatambua mchango wa masheikh na maimamu na watu mbalimbali wanaotoa mawaidha, lakini amewataka kuzingatia misingi ya lugha katika michango yao.
Sheikh Zubeir amewasisitizia masheikh, maimamu na watoaji wa mihadhara na kuangalia njia sahihi ya utoaji wa mawaidha kwa kuangalia misingi ya lugha yenye staha ili kuwaweka waumini katika mazingira mazuri.
Wakati huo huo Mufti Zubeir aliwatakia watanzania mwaka mpya mwema na kuendelea kudumisha amani iliyopo.