24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Mgombea urais ashindwa kupiga kura

lyimoNA UPENDO MOSHA, MOSHI

MGOMBEA wa urais kwa tiketi ya Tanzania Labour Party (TLP), Macmilan Lyimo, jana alishindwa kupiga kura baada ya kufika katika kituo cha kupigia kura kilichopo Kata ya Njia Panda, Wilaya ya Moshi, Mkoani Kilimanjaro, akiwa hana kitambulisho chake cha kupigia kura.

Mgombea huyo ambaye ni miongoni mwa wagombea wanane wanaowania kiti cha urais katika uchaguzi mkuu uliofanyika jana, alifika katika Kituo cha Ghalani, saa tatu asubuhi kwa lengo la kupiga kura, lakini hakufanikiwa, licha ya kuwapo kwa fomu maalumu namba 19  ambayo mgombea alipaswa kujaza ili kuruhusiwa kupiga kura  kutokana na kutokuwa na kitambulisho cha kupiga kura.

Akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na tukio hilo, Lyimo alisema alijiandikisha jijini Dar es Salaam.

Pamoja na hayo, alisema aliamua kuja kupiga kura mkoani Kilimanjaro, lakini kwa bahati mbaya alisahau kitambulisho cha kupigia kura.

“Kweli nimezuiliwa kupiga kura na wasimamizi wa uchaguzi kwa kuwa nimesahau kitambulisho cha kupiga kura kule Dar es Salaam,” alisema Lyimo.

Aliwataka wananchi katika majimbo ya Mkoa wa Kilimanjro na maeneo mengine nchini, kupiga kura kwa amani  kwa kuwachagua viongozi wenye moyo wa dhati wa kuwatumikia, ikiwa ni pamoja na kusubiri matokeo kwa hali ya utulivu.

Naye Msimamizi wa Uchaguzi katika kituo hicho, Aliko Mkumbwa, alithibitisha kushindwa kupiga kura mgombea huyo na  kumtaka kufuata taratibu za Tume ya Taifa ya Uchaguzi ili aweze kutimiza haki yake ya kikatiba ya kupiga kura.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles