24.8 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Magufuli: Majipu yakinishinda bora niache urais

RAis MagufuliNA ABRAHAM GWANDU ARUSHA

RAIS Dk. John Magufuli, amesema kama atashindwa kutumbua majipu dhidi ya wazembe na wabadhirifu serikalini, hana sababu ya kuendelea kushika wadhifa huo.

Amesema endapo hali hiyo ikitokea ni bora arudi nyumbani kwake akalale, kwa sababu lengo lake la kuwapatia wananchi Tanzania mpya, litakuwa halijatimia.

Rais Dk. Magufuli aliyasema hayo jana, wakati wa hafla ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa barabara ya Arusha-Holili yenye urefu wa kilometa 234.3, itakayogharimu Sh bilioni 209.3

“Ndugu zangu kazi hii ni ngumu, wapo watu ambao hawataki mimi na Serikali yangu kuwatumbua, nitapambana hadi nihakikishe ninafanikiwa.

“Na iwapo nitashindwa hakuna sababu ya mimi kuendelea kuwa Rais wa nchi hii, ni bora nirudi nyumbani kwangu kulala,” alisema.

Dk. Magufuli alisema amejitoa sadaka kwa ajili ya Watanzania na hivyo amewakumbusha wananchi waendelee kumwombea kwa Mungu, ili akamilishe kazi hiyo ngumu.

Alisema amekuwa akipata vikwazo wakati wa kutumbua majipu, katika hatua mbalimbali anazochukua dhidi ya watumishi wa umma wanaotumia vibaya madaraka yao.

“Tanzania ilikuwa imegeuka kuwa shamba la bibi, ilikuwa nchi ya ovyo kweli kweli, nimejitosa kuwa sadaka ya Watanzania, nihakikishe kuwa nitawavusha kutoka katika lindi kubwa la umasikini linalowakabili wananchi wa pato la chini,” alisema.

Rais Dk. Magufuli ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), amewataka wakuu wenzake wa nchi wananchama wa jumuiya hiyo kuhakikisha wanatimiza wajibu waliokabidhiwa na wananchi ili kuwasaidia kutoka kwenye umasikini.

Alisema umefika wakati viongozi wa nchi wanachama kuamka na kufanya kazi kwa bidii kwa lengo la kuwanufaisha wanachi wao ambao wengi wanateseka na umasikini, wakati nchi zao zimejaliwa rasilimali nyingi ikiwemo madini, mbuga za wanyama, gesi asilia, mafuta,misitu na ardhi nzuri kwa ajili ya kilimo.

Alisema barabara hiyo ikikamilika, itaharakisha maendeleo ya wananchi wa nchi wanachama katika nyanja za kilimo, biashara, viwanda na usafirishaji.

“Tutakapokamilisha barabara hii, tutaendelea na ujenzi wa barabara zitakazounganisha nchi zote za Jumuiya ya Afrika ya Mashariki, tuunganishe Tanzania na Rwanda na Burundi, tuunganishe Tanzania na Uganda na hatimaye mtandao wa barabara uziunganishe nchi zote sita” alisema Rais Dk.Magufuli.

Alisema kati ya fedha hizo, Sh bilioni 190 zimetolewa na Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Japan (JICA), huku kiasi cha Sh bilioni 19.4 zikitolewa kwa pamoja kati ya Serikali ya Tanzania na Jumuiya ya Afrika ya Mashariki.

“Lengo la nchi zetu ni kujitegemea, ndiyo maana kwa kiasi tunatumia fedha zetu za ndani, hatutaki tabia ya kuombaomba kwa vile tunazo rasilimali za kutosha, tukizitumia vizuri tutajitegemea” alisisitiza Rais Magufuli.

SUDAN KUSINI

Kuhusu hatua ya kuikaribisha Sudan Kusini kuwa mwanachma wa jumuiya hiyo, alisema nchi hiyo imekaribishwa baada ya pande hasimu zilizokuwa zikigombana kupatana na kumaliza vita ya wenyewe kwa wenyewe.

“Nchi ya Sudan Kusini ni nchi tajiri sana, ina zaidi ya aina 22 za madini na vito vya thamani, inaongoza kuwa na mifugo mingi katika jumuiya yetu, uroho wa madaraka waliokuwa nao viongozi umechangia wanachi wa nchi hiyo kuwa masikini na mimi nawaambia kuwa lazima watambue madaraka yanatoka kwa Mungu” aliasa Rais Magufuli.

RAIS KENYATA

Kwa upande wake Rais wa Kenya, Uhuru Kenyata, alisema umefika wakati kwa nchi za jumuiya hiyo kuondoa vikwazo vyote katika mipaka ya nchi zao ili kurahisisha biashara zinazofanywa na wananchi wa nchi hizo .

Aliwataka viongozi wenzake kuweka mkakati wa pamoja wa kuanzisha viwanda vipya na vya kisasa ili kuachana na vile vilivyoachwa na wakoloni na kutoa ajira kwa vijana ambao wengi wamesoma na wanakimbilia nchi za nje kwenda kutafuta kazi.

“Hatuna haja ya kuagiza nguo za mitumba kutoka nje ya nchi zetu, hatuna haja ya kuagiza samani za ndani, magari, pamoja na bidhaa zingine ambazo kwa mali ghafi tulizonazo tunaweza kuzitengeneza” alisema Rais Kenyata.

Amesema kuna haja ya nchi za Afrika ya Mashariki kusimamia uchumi wake na kuachana na tabia ya kuajiri wazungu na kwamba kama wazungu wanataka kuja Afrika waje kwa ajili ya utalii na si kuja kutuletea nguo na magari.

RAIS MUSEVENI

Naye Rais wa Uganda, Yoweri Museveni alisema nchi hizo zinakosa maendeleo pamoja na kuwa na rasilimali nyingi kutokana na wananchi wengi kukosa huduma muhimu za afya na elimu.

“Tunao wajibu wa kusimamia na kuwaelimisha wananchi wetu ili waweze kutumia ardhi nzuri kwa kilimo cha kisasa kitakachowezesha kuzalisha chakula na ziada kwa ajili ya biashara na kukuza uchumi wa watu wetu.

“Barabara hii ikikamilika itanufaisha wananchi wetu , watasafirisha mazao yao kutoka hapa Arusha kwenda Taveta na Mombasa huko Kenya, itumieni vizuri pindi itakapokamilika” alisema.

Baadhi ya viongozi na wawakilishi kutoka nchi mbalimbali waliohudhuria hafla hiyo, ni pamoja na Balozi wa Japan nchini Tanzania, Masaharo Yoshida, Makamu wa Pili wa Rais wa Burundi, Dk.Joseph Butore, Makamu wa Pili wa Rais wa Sudan Kusini, James Igga, Mwakilishi wa Rais wa Rwanda, Valentine Rwegabure na Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles