24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

KUELEKEA UCHAGUZI MKUU TFF 2017: WAJUE WAGOMBEA

Salum Chama (Ujumbe)

Alizaliwa mwaka 1960 mjini Bukoba na kufanikiwa kuhitimu elimu ya darasa la saba mwaka 1974 katika Shule ya msingi Bukoba.

Mwaka 1978, alihitimu kidato cha nne katika Shule ya Sekondari ya Bukoba, wakati akiwa kidato cha pili mwaka 1976. Alichaguliwa kuwa mchezaji wa soka katika kombaini ya shule za sekondari za Mkoa wa Kagera (Bwikano).

Baada ya kuhitimu masomo ya sekondari, aliajiriwa katika Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) Manispaa ya Bukoba kama mtunza fedha.
Nafasi hiyo ilimwezesha kupata ajira katika timu ya Balimi ya Bukoba mwaka 1979, ambayo aliitumikia hadi mwaka 1984 alipoamua kustaafu kucheza soka.

Mwaka 1985 aligeukia uamuzi wa soka na kupanda hadi daraja la kwanza, ambako alichezesha michezo mingi kwa wakati huo na kujikuta akichaguliwa kuwa Katibu wa Chama cha Soka cha Wilaya ya Bukoba mwaka 1989.

Chama aliendelea na harakati zake katika mchezo wa soka, huku mwaka 1990 akichaguliwa kuwa Katibu Msaidizi wa Chama cha Soka Mkoa wa Kagera.

Licha ya kuwa na jukumu katika chama hicho, mwaka 2000 alijitosa kugombea na kushinda udiwani kata ya Bilele Manispaaa ya Bukoba, ambapo aliweza kudumu kwenye nafasi hiyo hadi mwaka 2012 alipochaguliwa kuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Soka cha Mkoa wa Kagera.
Mwaka 2013 alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Waamuzi na mwaka 2016 aligombea tena na kushinda nafasi ya Katibu Mkuu wa Chama soka Mkoa wa Kagera hadi sasa.

 

Saad Kawemba (Ujumbe)

Kawemba alianza kujihusisha na masuala ya soka tangu akiwa na umri wa miaka 12 mwaka 1981 katika kituo cha ‘Black Fighter Kids’.

Mwaka 1986 alipandishwa ‘Black Fighter FC na kufanikiwa kujiunga na timu ya Halmashauri SC ya mkoani Kigoma mwaka 1988, kikosi hicho kiliweza kutwaa ubingwa wa mkoa.

Kawemba alimaliza elimu yake ya kidato cha nne mwaka 1988 katika Shule ya Sekondari ya Kigoma na kuendelea na elimu ya juu ya kidato cha tano katika Shule ya Sekondari ya Azania na kuhitimu mwaka 1990.

Mwaka 1991 alijiunga na timu ya JKT Mafinga akiwa jeshini kwa mujibu wa sheria, ambapo alicheza kwa muda wa mwaka mmoja, huku akifanikiwa kusajiliwa na kuichezea timu ya daraja la kwanza ya Sigara SC mwaka 1992 hadi 1993.

Ndoto za kuendelea kuutangaza mpira wa miguu hazikuweza kuishia hapo, kwani alibahatika kupata ufadhili wa kwenda kusoma katika chuo cha Islamic nchini Uganda, ambapo mwaka 1994 alikuwa miongoni mwa wachezaji waliofanikisha ushindi wa ubingwa katika chuo hicho kwenye mashindano ya vyuo vikuu vya mashariki.

Mwaka 1995 alimaliza Shahada ya Kwanza ya Kufundisha Sayansi (BSC) chuoni hapo na kuendelea kufundisha kama mkufunzi chuoni hapo.

Mwaka 1997 alichaguliwa kuwa mwalimu wa michezo, nafasi aliyoweza kudumu hadi alipopata nafasi ya kufanya kazi katika Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) mwaka 2007.

Kawemba alipata nafasi ya kuwa Ofisa Takwimu wa Shirikisho hilo mwaka 2010 na kuchaguliwa kuwa Mkurugenzi wa mashindano, ambapo nafasi hiyo aliitumikia hadi mwaka 2014, alipoamua kujiunga na Azam FC kama Ofisa Mtendaji Mkuu wa klabu hiyo hadi Juni mwaka huu.

 

JAMAL MALINZI (URAIS)

Malinzi alizaliwa mwaka 1960 mkoani Kagera na kumaliza elimu ya msingi mwaka 1977.

Mwaka 1978 alijiunga na Shule ya Sekondari Mwanza na kuhitimu kidato cha nne mwaka 1980 na kupata nafasi ya kuendelea na elimu ya kidato cha tano na sita katika Shule ya Ilboru kuanzia mwaka 1981 hadi 1982.

Baadaye Malinzi alijiunga na kambi ya Ruvu kwa ajili ya mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa, huku mwaka 1981 hadi 1985 akichaguliwa kuwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM) akisomea Shahada ya Uhandisi.

Ameweza kufanya kazi katika Kampuni ya ‘Coopers and Lybrand Tanzania Industrial Research and Development Organization’ mwaka 1986 hadi 1993.

Alijiunga rasmi katika ulimwengu wa soka mwaka 1995 na kuwa promota wa ngumi za kulipwa, kazi aliyoifanya kwa kipindi cha miaka sita.

Moja ya mabondia wanaojivunia nafasi ya Malinzi ni Rashid Matumla ambaye ameweza kulitangaza Taifa katika mapambano ya kitaifa na kimataifa.
Mwaka 1999 hadi 2005, Malinzi alifanikiwa kushika nyadhifa mbalimbali katika mchezo wa soka, ikiwamo Seneta wa Yanga, Mkurugenzi wa klabu hiyo kabla ya kuteuliwa kuwa Katibu Mkuu chini ya Mwenyekiti Francis Kifukwe.

Mbali na Yanga, Malinzi amewahi kuwa Mkurugenzi na Msimamizi Mkuu wa timu ya soka ya Mkoa wa Dar es Salaam Mzizima United, pia ameweza kuwa mjumbe wa Baraza la Michezo Mkoa wa Dar es Salaam mwaka 2009 hadi 2011, wakati huo akiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano Mkoa wa Pwani.

Malinzi ni Mwenyekiti wa Chama cha Soka Mkoa wa Kagera na Rais anayemaliza muda wake katika Shirikisho la Soka Tanzania, nafasi aliyoweza kuishika tangu mwaka 2013, baada ya uongozi uliokuwa chini ya Leodegar Tenga kumaliza muda wake.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles