Na Sheila Katikula, Mwanza
Manispaa ya Ilemela inapoteza zaidi ya Sh milioni 80 kwa mwaka kwa sababu ya kutoboresha miundombinu ya soko kuu la Wilaya la Kiloleli lililopo wilayani Ilemela jijini mkoani Mwanza.
Hayo yamesemwa Septemba 17, na Diwani wa Kata ya Ibungilo, Hussein Magera wakati akizingumza na Mtanzania Digital ofisini kwake na kuweka wazi kuwa mfumo wa uendeshaji wa kimasoko haujafanyika katika soko hilo na kupelekea kupoteza fedha nyingi kutoka katika eneo hilo.
Alisema ni vema halmashauri kutenga fungu la kuboresha miundo mbiu katika soko hilo kwani mpaka hivi sasa mazingira siyo rafiki kwa sababu hakuna uzio kwenye eneo hilo na kuona umuhimu wa kutenga fedha ambazo zitajenga uzio na maeneo ya kuegesha magari kusaidia kupata fedha kutoka kwa wafanyabiashara hao.
Alisema inasikitisha kuona watu wanafanya biashara pembeni ya barabara za lami na kuacha masoko yakiwa wazi hali ambayo ni upotevu wa mapato ya halmashauri hivo ni vema serikali kurudusha nyuma fikra na kuboresha masoko yaliyopo kila sehemu ili waweze kupata mapato.
Naye Mwenyekiti wa soko la Kiloleli, Modesti Simfukwe alisema soko hilo lina uwezo kwa kuchukua wafanya biashara wengi kwani lina vizimba  vya ndizi 100, maduka 140, vibanda vya mbao 930 vya chuma.
Simfukwe alimuomba mkuu wa mkoa kuwashirikisha machinga wote itakapofika siku ya kuwapanga upya kama ilivyoelekezwa na Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu.