MWANDISHI WETU-DAR ES SALAAM
MKUU wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Simon Sirro, amefanya mabadiliko madogo kwa kumteua Naibu Kamishna wa Polisi (DCP), Ahmed Msangi kuwa Naibu Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Zanzibar.
Kabla ya uteuzi huo, Msangi alikuwa Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Msemaji wa Jeshi la Polisi na nafasi yake imechukuliwa na Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP), David Misime.
Taarifa iliyotolewa na Kamishna wa Ushirikishwaji wa Jamii, Mussa Mussa, ilieleza kuwa katika mabadiliko hayo aliyekuwa Naibu Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Zanzibar, Maulid Mabakila, amehamishiwa makao makuu ya polisi Dar es Salaam.
Wakati wa makabidhiano ya ofisi, DCP Msangi alisema mabadiliko hayo ni ya kawaida katika kuboresha utendaji wa Jeshi la Polisi na kuwaomba waandishi wa habari kuendelea kushirikiana nalo.
Msemaji mpya wa jeshi hilo, SACP Misime, aliwaomba waandishi wa habari na wananchi kuendeleza ushirikiano katika kuelimisha jamii kuachana na vitendo vya kujichukulia sheria mkononi.