Waziri wa Afya, Maendeleo ya jamii, jinsia, Wazee na watoto, Ummy Mwalimu, ameitaka jamii kujitoa kusaidia matibabu ya watoto wanaosubiri kutibiwa katika Taasisi Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI).
Akizingumza leo April 28, katika mbio za kuchangisha fedha za matibabu ya moyo ya watoto 200, Ummy amesema jamii ijenge utamaduni wa kushirikiana na JKCI kuwasaidia kupata matibabu .
Amesema taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na wadau wengine wanaokuwa tayari katika kuchangia matibabu hayo kwa ajili ya kuokoa maisha ya watoto nchini.
Naye Mkurugenzi wa Taasisi ya JKCI, Professa Mohamed Janabi, amesema fedha zinazohitajika ni sh milioni 200 kwa watoto 200 pekee wanaotakiwa kufanyiwa matibabu ya Moyo.
“Wakitibiwa hao 200, watoto wengine 512 wataendelea kusubiri kupatiwa matibabu hayo.
“Niiombe jamii kuwa maradhi haya ya moyo ni makubwa hivyo mle kwa wastani na kufanya mazoezi ya kukimbia kusudi kuepuka maradhi haya,” amesema professa Janabi.
Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Mazingira, kutoka Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (Dawasa), Mhandisi Modesta Mushi, ambaye alishiriki mbio hizo za Kilomita 10, pamoja na kuchangia damu alisema watoto hao ni sehemu ya jamii hivyo Dawasa watajitoa kuokoa maisha yao.
“Dawasa tumeshiriki kama wadau na wazazi katika ngazi ya familia, nimeona kuna umuhimu mkubwa wa kuchangia damu kwa kuwasaidia waliopo vitandani huko Hospitali,” alisema Modester.