MBUNGE wa Singida Mashariki, Tundu Lissu amekamatwa na polisi akiwa nyumbani kwake mjini Dodoma na kusafirishwa jijini Dar es Salaam leo kwa madai ya kuvunja masharti ya dhamana.
Lissu alikamatwa leo saa tano asubuhi wakati akijiandaa kwenda kwenye kesi dhidi ya Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS) na Mwanasheria Mkuu wa Serikali iliyofunguliwa na Godfrey Wasonga mjini humo ambapo mahakama ilikuwa isikilize kesi ya msingi na maombi ya zuio la uchaguzi wa rais wa TLS hadi kesi hiyo itakapomalizika kama iliyoombwa na Wasonga.
Kamanda wa Polisi Mkoani humo, Lazaro Mambosasa amethibitisha kukamatwa kwa Lissu huku akitaja sababu kuwa ni maagizo kutoka Kanda Maalumu ya Dar es Salaam.
“Tumemkamata saa tano asubuhi nyumbani kwake eneo la Area D, na mara baada ya kumkamata amesafirishwa kuelekea jijini Dar es salaam, sababu nyingine mimi sijui ninachojua ni kwa maagizo tuliyopewa kutoka kanda hiyo,” amesema.
Hata hivyo, Wakili Peter Kibatala amesema maombi ya zuio la kusimamishwa kwa uchaguzi hadi kesi hiyo itakapomalizika yametupwa, hivyo uchaguzi wa TLS uko pale pale.