25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

WAZIRI NAPE: NITAJIUZULU

*Ni ikibainika ana uhusiano na Wema Sepetu


Na ELIZABETH HOMBO-DAR ES SALAAM

WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye, amesema atajiuzulu uwaziri endapo mtu atampelekea ushahidi wa kuwa na uhusiano wa kimapenzi na msanii yeyote.

Kauli hiyo ya Nape inakuja ikiwa ni takriban wiki tatu tangu Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, aseme watu wanaotetea wale aliowataja hadharani kwa kuhusika na dawa za kulevya wengine ni wapenzi wao.

“Wengine wanaumia tunagusa wapenzi wao, wawasaidie waache si kupiga kelele tu, ujumbe umefika,” alisema Makonda katika moja ya mikutano yake.

Ingawa katika mkutano huo Makonda hakumtaja mtu kwa jina, lakini aliitoa kauli hiyo siku chache baada ya Nape kupinga mfumo wake wa kutaja majina ya watu hadharani, hususani wasanii na kuwatuhumu kuhusika na dawa za kulevya.

Nape alisema kuwataja watu bila ushahidi ni kuwachafulia majina yao waliyoyatengeza kwa muda mrefu.

Mbali na Nape, Mbunge wa Geita Vijijini, Joseph Msukuma (CCM), alizungumza mara kadhaa bungeni akimpinga Makonda kwa mfumo wake aliokuwa akitumia, kutaja majina ya watu wanaojihusisha na dawa za kulevya.

Akizungumza katika kipindi cha Dakika 45 kinachorushwa na kituo cha luninga cha ITV juzi, Nape alieleza kushangazwa na kitendo cha kuhusishwa kuwa na mahusiano na wasanii.

“Ila kama mtu ana ushahidi alete hapa mezani aseme Nape hili unalofanya, unafanya kwa sababu una uhusiano, na mtu akileta najiuzulu uwaziri.

“Hii ni katika watu ambao wanakosa hoja halafu wanasingizia hoja ambazo hazina msingi, ningefurahi mtu akisema Nape hana sababu ya kutumia busara, twende na hoja hii nyingine ni upuuzi,” alisema Nape.

Akizungumzia kuhusu kutajwa kuhusishwa kuwa na mahusiano ya kimapenzi na msanii nyota wa filamu, Wema Sepetu, Nape alisema wasanii wengi ni wadogo zake akiwamo Wema.

“‘Majority’ ya wasanii hawa ni wadogo zangu. Wamezungumza habari ya Wema, sasa nieleze ukweli kwamba baba yake, mzee Sepetu (Isack) na baba yangu (Moses Nnauye) ni mtu na kaka yake, kwa hiyo Wema ni mdogo wangu sana sana.

“Mama yake anatoka Singida, mama yangu naye anatoka Singida, ni mtoto mdogo lakini mtu akiamua apoteze ‘direction’ (mwelekeo) ya mjadala anaweza kuja na hoja nyingi sana.

“Mimi nimeanza kufanya kazi na wasanii, nimefanya nao kazi kwa miaka 16, hii ya uwaziri imekuja juzi tu. Pia msisahau hawa wasanii tuliwatumia kwenye kampemi ya CCM, mimi ndiyo nilikuwa Katibu wa Uenezi wa CCM.

“Ukizungumza burudani, hamasa na ‘publicity’ mimi ndio nashughulika nayo, hivyo kuwaingiza wasanii kwenye kampeni haikuwa kazi rahisi, sasa nikiwa nao karibu dhambi inatoka wapi, maana ndio nilipewa dhamana ya kuwasaidia. Hizi hoja zingine ni za kijinga kabisa,” alisema Nape.

Pamoja na mambo mengine, Nape alisema utaratibu uliokuwa ukitumiwa na Makonda kwa kutaja majina ya watu hadharani una madhara makubwa kwani unajenga chuki katika jamii.

Nape ambaye pia ni mbunge wa Mtama mkoani Lindi, alisema hakuna mahali popote duniani vita ya dawa za kulevya ilishinda kwa kupiganwa hadharani.

 “Tutajenga chuki kubwa sana kwenye jamii kama tukianzisha utaratibu wa kila mtu anasimama anamtaja mtu hadharani, ukishamtaja anaandikwa kwenye mitandao.

“Nchi itaingia kwenye vurugu kubwa bila sababu na wale wenye chuki zao watapitia hapo kuanza kutajana majina, tukitajana majina hadharani, hii vita hakuna mahali walipigana hadharani wakashinda popote duniani, haipo,” alisema.

Waziri huyo alisema vita hiyo itashinda iwapo itapiganwa kimya kimya, kwa sababu wanaofanya biashara hiyo hawafanyi hadharani bali wanafanya kwa kificho.

“Shughulika nao kwa kificho, mwiba unapoingilia ndipo unapotokea, usitake kuutolea sehemu nyingine. Mtu anapita kwa kificho, ukishamkamata hata ukimtangaza hadharani lakini umeshamkamata… unaenda kuwinda unapiga risasi hewani, wanyama wote watakimbia.

“Kwa hiyo shida yangu ilikuwa inaniuma, kwamba wale hasa ambao tuna tatizo nao watakimbia. Nikasema lazima tutumie busara. Lingine nikazungumzia kuhusu ‘brand’, gharama ya kutengeneza ‘brand’ ni kubwa. Sasa anapokuja mtu akakwambia unajihusha na dawa za kulevya lazima ataua ‘brand’ yako. Ikishaharibika kuitengeneza ni kazi.

“Nikasema tutumie busara. Ukimtuhumu mtu mkubwa sisi kama Serikali lazima tufanye kazi ya kuzilea hizi ‘brand’. Nikasema hawa wasanii wangu wametajwa mle ndani, mimi sitaki kuwatetea, lakini ili tumtaje kwanini tusichunguze mpaka tukamkamate?

“Humu ndani wapo wanasiasa wakubwa, ni kweli hoja ipo kwamba tusijali ukubwa, sura zao, umaarufu wao. Mimi nasema umaarufu usitumie kuwalinda, lakini umaarufu au sura zao zitufanye sisi tuwe makini zaidi kushughulika nao.

“Lakini mwisho wa siku tuwe na uhakika kuwa huyu tunampeleka mahakamani anahusika kuliko tunampeleka mahakamani au tunamtia ndani halafu tukikuta hajakosea, namna ya kurudisha ‘status’ yake inakuwa ngumu,” alisema Nape.

Aidha alisema watu wasihukumiwe bila kosa bali haki itendeke na sheria na taratibu zifuatwe.

“Namshukuru Rais (Dk. Magufuli) ametumia busara namna ya kuli-handle (kulishughulikia) hili suala, amemteua kamishna na amemkumbusha waziri mkuu kwamba yeye ndie mwenyekiti wa hii kamati na mawaziri wako ndio wajumbe, sasa ameweka vita hii katika chombo salama.

“Pia namshukuru kamishna mwenyewe kasema tusitaje majina hadharani, lakini tufuate sheria na akasema hakuna jiwe litabaki juu ya jiwe, tutahakikisha tunasimamia sheria,” alisema Nape.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles