23.3 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Watanzania 85 wasubiri kunyongwa China

CHRISTINA GAULUHANGA-DAR ES SALAAM

MAMLAKA ya Kuzuia Dawa za Kulevya nchini, imesema Watanzania 85 wanatarajiwa kunyongwa Hong Kong nchini China baada ya kupatikana na hatia ya kujihusisha na biashara haramu ya dawa za kulevya.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, Kaimu Kamishna Jenerali wa mamlaka hiyo, James Kaji, alisema Watanzania hao walihukumiwa kwa sheria ya nchi hiyo ambayo mtu akipatikana na hatia katika makosa ya dawa za kulevya adhabu yake ni kunyongwa.

Alisema pia Watanzania 265 walikamatwa nchini humo kwa kosa hilo na tayari 130 wamehukumiwa.

“Ni jambo la kusikitisha kwakuwa vijana hawa wengi wao wanachukuliwa hapa nchini na wafanyabiashara wakubwa kwa kisingizio cha kufanya kazi za ndani, lakini wengi wao wanatumika kwenye ukahaba na kusafirisha dawa hizi za kulevya,” alisema Kaji.

Alisema wakati sasa umefika kwa jamii kuhakikisha inawalinda watoto wao ipasavyo na kuzuia wasisafirishwe nje ya nchi kwa manufaa ya watu wengine kwakuwa wanauza utu wao na kuhatarisha maisha yao.

BANGI NCHINI

Akizungumzia kuhusu mjadala ulioibuka bungeni juzi kuhusu kuruhusu kilimo cha bangi nchini, Kaji alisema mamlaka hiyo haipo tayari kuruhusu kilimo hicho kwakuwa kina madhara na hadi sasa bado wanaendelea kuwasaka wanaojishughulisha na zao hilo ikiwamo Mkoa wa Mara.

Alisema tayari bangi imeonyesha madhara ndani ya jamii na wamekuwa wakiendelea na operesheni ya kukamata watumiaji na wakulima wa zao hilo, hivyo kuruhusu kilimo hicho kunaweza kuwachanganya kiutendaji.

Aliongeza kuwa wanatambua wanaojihusisha na biashara hiyo wamekuwa wakitumia mbinu tofauti na kwa sasa wengi wanaficha kwenye saruji nyeupe na kwenye gari nyingi zinazoingia nchini kutoka nchini Japan.

Wakati huohuo, mamlaka hiyo inawashikilia vijana Stanley Ngowi (24), mkazi wa Tabata Segerea na Sultan Ngowi (24), mkazi wa Kinondoni kwa tuhuma kusafirisha dawa za kulevya.

Alisema watuhumiwa hao walikamatwa maeneo ya Kibo Ubungo, Januari 27, mwaka huu wakiwa na gari aina ya Sienta rangi ya silva yenye namba za usajili T 776 DSE.

Alisema watuhumiwa hao walikamatwa wakiwa na unga ambao baada ya uchunguzi wa maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali ilithibitika ni dawa za kulevya aina ya heroini wenye uzito gramu 508.163.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles