25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

WADAIWA SUGU NHC WANAJIAIBISHA

nhc

SHIRIKA la Nyumba la Taifa (NHC) limewasilisha ripoti ya wadaiwa wake sugu zikiwamo wizara, taasisi za Serikali na watu binafsi kwa Rais Dk. John Magufuli, huku wizara mbili zikiwa na deni kubwa.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam Jumatano wiki hii, Mkurugenzi wa Mikoa na Utawala wa NHC, Raymond Mndolwa, alisema uamuzi huo umekuja baada ya Rais Dk. Magufuli kuwataka kukusanya madeni hayo na kuwasilisha taarifa hiyo ofisini kwake ili aweze kuipitia.

NHC ilitoa notisi ya siku 90 ambayo ilianza  Septemba, mwaka huu, huku wadaiwa hao wakitakiwa kulipa madeni yao ndani ya muda uliopangwa.

Kwamba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee, Jinsia na Watoto na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo zinadaiwa kiasi kikubwa cha fedha, licha ya kuwapo kwa mazungumzo ya kulipa madeni yao.

Kwamba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee, Jinsia na Watoto inadaiwa Sh bilioni 1.4, wakati wamelipa Sh milioni 300; wakati Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo inadaiwa Sh bilioni 1.14, lakini imelipa Sh milioni 700 tu.

Kwamba shirika hilo hadi sasa limekusanya Sh bilioni 5.9 kati ya Sh bilioni 9.3 ambalo ni deni la Serikali kupitia wizara na taasisi mbalimbali, huku Sh bilioni 2.5 zikikusanywa kutoka kwa wadaiwa binafsi ambao awali walikuwa wanadaiwa Sh bilioni 4.

Kwamba lengo la shirika hilo ni kuhakikisha madeni yanalipwa ili fedha hizo ziweze kutumika katika shughuli nyingine za maendeleo, ikiwamo ujenzi wa nyumba za kisasa 300 mkoani Dodoma.

Wizara nyingine zinazodaiwa ni Wizara ya Katiba na Sheria, Wizara ya Fedha na Uchumi, Wizara ya Uchukuzi, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi na iliyokuwa Wizara ya Ujenzi.

Kwamba wadaiwa wengine ni Ofisi ya Waziri Mkuu, Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC).

Tunasema kama wizara ndizo zinadaiwa, ina maana kuwa Serikali ndiyo inadaiwa wakati ni wajibu wake kulipa madeni ipasavyo.

Kwamba wizara ndizo zinapaswa kutoa mifano kwa taasisi binafsi kwa kulipa madeni yake ili taasisi hizo ziige mifano hiyo mizuri.

Tunasema wizara hizi, ambazo kimsingi ni Serikali, zinapaswa kuwa chachu kwa taasisi za binafsi kwa kuwa mfano katika kulipa madeni yake.

Tunasema kuwa wizara nyeti kama Wizara ya Katiba na Sheria, Wizara ya Fedha na Uchumi, Wizara ya Uchukuzi, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi na iliyokuwa Wizara ya Ujenzi, Ofisi ya Waziri Mkuu, MNH na TPDC ni wizara na taasisi zenye heshima. Tunasema zidumishe heshima zake kwa kulipa madeni yake kwa wakati.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles