24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

SIYO KILA MTU ANAFAA KUWA MENEJA WA MSANII

babu-tale

Na JOSEPH SHALUWA

Hakuna ubishi kuwa mafanikio ya msanii yanategemea zaidi juhudi, ubunifu na kufanya kazi kwa kujituma zaidi. Msanii bila kuwa na juhudi binafsi, kuumiza kichwa ili kupata vitu vipya kwa mashabiki wake, hawezi kudumu muda mrefu kisanii.

Tumeshuhudia wasanii wenye ubunifu wakiwa na mafanikio makubwa zaidi kuliko wale ambao wanafanya mambo yaleyale kila siku.

Mfano kwenye Bongo Muvi, ukiwaangalia wasanii kama Salum Ahmed ‘Gabo’, Jacob Stephen ‘JB’, Single Mtambalike ‘Richie’, Yusuph Mlela, Rose Ndauka na Ndumbangwe Misayo ‘Thea’ ni alama ya wasanii wenye juhudi binafsi kwenye uigizaji.

Ukirudi kwenye muziki utakutana na wasanii kama Ali Kiba, Omari Nyembo ‘Ommy Dimpoz’, Nasibu Abdul ‘Diamond’, Hamisi Mwinjuma ‘Mwana FA’, Farid Kubanda ‘Fid Q’ nao wanawakilisha kundi la wasanii wanaofanya vizuri kwenye Bongo Fleva.

Pamoja na juhudi, kujituma, ubunifu na mengine mengi muhimu ambayo yanaweza kumuacha msanii kwenye kilele cha mafanikio muda mrefu, suala la menejimenti ni muhimu sana kwa msanii husika.

Tunaona hata wasanii wa nje, wengi wana mafanikio makubwa kutokana na kuwa chini ya uongozi wa mameneja makini.

Hapa kwetu Tanzania tunaona kuna baadhi ya wasanii wana mameneja, wengine wanawatumia vizuri lakini wengine hali zao ni mbaya.

Upo ushahidi juu ya wasanii wenye mameneja wazuri na mafanikio yao makubwa katika kazi zao. Mfano mzuri ni msanii Diamond, ambaye ana timu ya mameneja ambao wamegawana majukumu na kwa hakika wanamsaidia sana.

Kuna wasanii wana mameneja lakini mafanikio yao ni sifuri. Hilo ni tatizo. Wapo mameneja ambao si wabunifu na kazi yao ni kufikiria matumbo yao.

Nawasihi wasanii wetu wa Tanzania waamke sasa. Si kweli kwamba kila mtu anaweza kuwa meneja. Kaa chini utafakari. Je, meneja uliyenaye/ulionao wanakusaidia kwa kiwango gani?

Kuna hatua unazopiga kutokana na usimamizi wa shughuli zako? Kumbuka wewe kama msanii, siyo kazi yako tena kuhangaikia suala la masoko, mitindo, mitoko nk. Lazima uwe na meneja ambaye atapanga vizuri watu wa kusimamia ratiba zako zote vizuri.

Meneja wako anafanya yote hayo? Umefanikiwa kwa kuwa mikononi mwake au upo naye ili uonekane tu kwamba na wewe una meneja? Kama una meneja na huoni mchango wake, ni vizuri mkaachana kwa amani, kisha ukatafuta meneja mwingine mwenye nia na uwezo wa kweli wa kusimamia kazi za sanaa.

Wengine ni wachumia tumbo tu. Ni kazi ya wasanii sasa kujitathimini na kuchukua hatua.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles