ISTANBUL, UTURUKI
MAJESHI ya Uturuki yameendeleza mashambulizi kaskazini mwa Syria licha ya ukosoaji kutoka mshirika muhimu, Marekani.
Marekani ina wasiwasi kutokana na makabiliano baina ya Uturuki ambayo ni mwanachama wa Jumuiya ya Kujihami (NATO), na wanamgambo wa Kikurdi inaowaunga mkono.
Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Ashton Carter, alisema wametoa wito kwa pande hizo kuacha kupigana na badala yake kulilenga kundi lijiitalo Dola la Kiislamu (IS).
Msemaji wa Wakurdi wa Syria, Shervan Darwish, aliishutumu Uturuki kulenga kuwaangamiza watu wa Kaskazini mwa Syria, ili kuwaweka watu wenye itikadi kali za Kiislamu.
Lakini Uturuki inawatilia shaka wanamgambo wa Kikurdi nchini humo, ikiwatuhumu kuwa na mfungamano na waasi wa Kikurdi ndani ya Uturuki.