24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

UTATA KUPIGWA RISASI KWA KIGOGO CCM

GORDON KALULUNGA- MBEYA


UTATA umeibuka baada ya Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Wilaya ya Mbeya Mjini, Ephrahim Mwaitenda, kunusurika kifo baada ya kupigwa risasi mgongoni na watu wasiojulikana.

Tukio la kupigwa risasi kwa kiongozi huyo wa chama tawala, lilitokea usiku wa kuamkia jana wilayani Kyela mkoani hapa, katika Kijiji cha Makwale. Alipigwa risasi akiwa anasali.

Akizungumza baada ya kupokewa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mbeya, Mwaitenda, alisema akiwa nyumbani kwake usiku alihisi vishindo vya watu nje ya nyumba yake hivyo alilazimika kuamka na kuanza kusali.

“Nilipomaliza kusali huku nikiwa na simu yangu ya kiganjani kando ya kitanda changu, nikasikia sauti ya mlipuko na kudhani ni simu yangu imenilipukia, ndipo nikatoa sauti ya kuomba msaada,” alisema Mwaitenda.

Alisema baada ya ndugu zake na majirani kuamka, waliingia chumbani na kukagua simu ambayo waliikuta ikiwa salama huku kioo cha dirisha la chumbani kikiwa kimepasuka na damu zikiwa zinamvuja.

Akithibitisha kupokewa kwa majeruhi huyo, Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mbeya, Dk. Fred Mbwanji, alisema walimpokea jana saa mbili asubuhi na madaktari walimpa matibabu kabla kumpeleka chumba cha x-ray ili kuweza kubaini risasi iliyokuwa mwilini kwa kiongozi huyo.

Kwa upande wake, Kaimu Katibu wa CCM Mkoa wa Mbeya, Zongo Lobe, alilaani tukio hilo na kusema kuwa wanaamini vyombo vya dola vitafanya kazi yake ili kuweza kuwatia mbaroni watu waliohusika na tukio hilo.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Dhahiri Kidavashari alipopigiwa simu ili kuzungumzia tukio hilo, alipokea mmoja wa wasaidizi wake ambaye alimtaka mwandishi kutuma ujumbe mfupi wa maandishi ambao hata ulipotumwa haukujibiwa hadi tunakwenda mitamboni.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles