NA MWANDISHI WETU, DAR ES SALAAM
SAKATA la upangaji wa matokeo katika michuano ya Ligi Daraja la Kwanza (FDL) iliyomalizika mwishoni mwa wiki iliyopita, limepelekwa kwenye Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa uchunguzi zaidi.
Juzi Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi iliyokutana kupitia taarifa za mechi mbili za Kundi C za ligi hiyo, ilishindwa kutoa uamuzi juu ya suala hilo la kinidhamu na kumtaka Katibu Mkuu wa TFF, Selstine Mwesigwa, alipeleke Kamati ya Nidhamu.
Timu za Kundi C zinazohusishwa na upangaji wa matokeo katika mechi za mwisho FDL ni JKT Kanembwa dhidi ya Geita Gold SC na Polisi Tabora dhidi ya JKT Oljoro.
Awali kabla ya sakata hilo kufikishwa kwenye Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi, TFF ilisimamisha matokeo na kugoma kutangaza timu itakayopanda daraja hadi taarifa zitakapopitiwa.
Hata hivyo, baada ya kamati hiyo ya saa 72 kupitia taarifa za mechi hizo na vielelezo vingine, ilionyesha mashaka kutokana na kuwepo viashiria vya upangaji wa matokeo.
Taarifa ya kamati hiyo ilieleza kwamba, kwa kuwa suala hilo ni la kinidhamu kwa mujibu wa ibara ya 50(1) na (11) ya katiba ya TFF na ibara ya 69 ya kanuni za nidhamu za shirikisho hilo, litaweza kufanyiwa uchunguzi na Kamati ya Nidhamu na kutolewa uamuzi.
Tayari TFF imetangza timu mbili zilizofanikiwa kupanda daraja na kucheza Ligi Kuu Bara msimu ujao ambapo Ruvu Shooting imefanikiwa kutoka kundi B na African Lyon kutoka kundi A.