23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Takukuru ichunguze, itoe ukweli wa fedha hizi

simon-chaula

MKURUGENZI wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Valentino Mlowola, ameombwa kufanya uchunguzi na kusema ukweli kuhusu tuhuma dhidi ya wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kupokea fedha.

Tunasema kuwa ukweli lazima usemwe ili kuondoa tetesi zinazosambaa kwa kasi kuwa wabunge wa CCM walipewa Sh milioni 10 kila mmoja ili kupitisha Muswada wa Sheria ya Huduma ya Habari 2016 uliotarajiwa kuwasilishwa katika Bunge linaloendelea sasa.

Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe, juzi alidai kuwa wabunge wote CCM wamehongwa kila mmoja Sh milioni 10.

Kwamba mgao wa fedha hizo uliratibiwa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, kwa kushirikiana na Katibu Msaidizi wa wabunge wa CCM, Abdallah Ulega.

Kwamba lengo la kutoa fedha hizo lililenga kuwalainisha wabunge hao ili wapitishe Mpango wa Maendeleo ya Taifa na Muswada wa Sheria ya Huduma ya Habari uliotarajiwa kuwasilishwa bungeni tangu jana.

Hoja hiyo aliibua bungeni juzi wakati wa kipindi cha maswali ya papo kwa hapo kwa Majaliwa.

Mbowe akiwa mbunge wa kwanza kupewa nafasi ya kumuuliza swali Majaliwa; aliuliza swali lakini Naibu Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson, alikataa lisijibiwe kwa madai kuwa halikuwa swali la kisera.

Mbowe alisema wabunge na mawaziri ni viongozi wa umma kwa mujibu wa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma namba 13 ya mwaka 1995, hivyo swali lake lilikuwa la kisera.

Kwamba kulikuwa na taarifa kuwa Oktoba 25, mwaka huu saa mbili usiku kiliitishwa kikao cha wabunge wa CCM huku Majaliwa akiwa mwenyekiti.

Kwamba katika kikao hicho ambacho kilihudhuriwa pia na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, zilitolewa fedha kwa wabunge wa CCM, wakiwamo mawaziri kiasi cha Sh milioni 10 kwa kila mmoja.

Kwamba fedha hizo zilitolewa kwa viongozi ambao wanabanwa na Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma na vilevile mgao huu uliendelea kutolewa katika ofisi za CCM makao makuu, ukiratibiwa na Ulega ambaye pia ni mbunge.

Mbowe alitaka Majaliwa ajibu kama taarifa hizo ziikuwa za kweli.

Lakini swali hilo liligonga mwamba baada ya Dk.Tulia kumzuia Majaliwa kulijibu. Mbowe alishikilia msimamo wake na kutaka swali hilo lijibiwe kwa kuwa linahusu sera.

Tunasema inabaidi Bunge lilitolee jibu bila kujali itikadi kutokana na hatua ya swali la Mbowe kuzuiliwa kujibiwa japo ni la kisera. Tunasema vilevile kuwa iundwe tume ya kimahakama ili kuchunguza suala la madai ya kutolewa fedha tajwa.

Tunapendekeza pia Takukuru ifanyie madai ya Mbowe uchunguzi kuwa kulifanyika kikao cha wabunge wa CCM Oktoba 25, mwaka huu baada ya Serikali kuona hasira za wabunge wao dhidi ya kudorora kwa uchumi, na Kinana na Majaliwa kukubaliana kuwapa fedha wabunge kiasi kilichofikia jumla ya Sh bilioni 2.7.

Tunasihi uchunguzi yakinifu ufanyike kuhusu suala hili na matokeo yake yaweze kutohojiwa ili kuiweka Serikali katika nafasi ya kuaminika kwa wananchi na kukomesha vitendo viovu kama kweli vilifanyika.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles