24.8 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

SIMU JANJA: KITU CHA KWANZA, MWISHO KUSHIKA KILA SIKU

Na MWANDISHI WETU

KILA mwaka takwimu za ndani na nje ya nchi zinaonesha kuongezeka kwa watumiaji wa mtandao wa intaneti.

Idadi hiyo imechangiwa na upatikanaji wa simu janja (smartphones) za bei nafuu. Ukitaka kuthibitisha hilo, hapo ulipo inua macho angalia mazingira uliyopo. Kama kuna watu wengine, kuna uwezekano mkubwa walio wengi wameshika simu za mkononi, macho kwenye vioo. Kwa sasa, simu janja ni kitu cha kwanza kushika asubuhi, kitu cha mwisho kushika kabla hujasinzia.

Kila kukicha watumiaji wa mtandao wanapoongezeka, inamaasha wateja wako wengi ambao wanatumia mtandao kufanya shughuli zao mbalimbali nao wanaongezeka. Je, kama mtoa huduma au bidhaa unaitumiaje fursa hii kuwafikia wateja wengi zaidi na kuongeza mapato ya biashara yako?

 

Kuna msemo usemao; ‘huwezi kuvua samaki stendi ya mabasi, au kusubiri meli kwenye uwanja wa ndege.’ Hii inamaanisha, kama ukitaka wateja wanaotumia mtandao kwenye shughuli zako za kila siku, ni vema kuhakikisha kwanza biashara yako nayo ipo mtandaoni.

Kuna njia kadhaa ambazo unaweza kutumia kuwafikia watu walioko mtandaoni. Kwanza ni kuwa na tovuti (website) maalumu kwa biashara yako. Miaka ya nyuma, tovuti zilikuwa ni maalumu kwa biashara kubwa pekee, lakini sasa huduma hizi zimerahisishwa na kuwa nafuu zaidi.

Mteja wako mtarajiwa haijui biashara au huduma unayotoa. Kikubwa atakachofanya ni kuitafuta kupitia njia mbalimbali kama vile Google kutafuta watoa huduma awatakao. Kuwa na tovuti yako, kutaifanya biashara hiyo ionekane na kukuongezea wateja zaidi.

Natambua wafanya biashara wengi hasa wadogo wamekuwa watumiaji wazuri wa mitandao ya kijamii hasa Instagram kutangaza biashara zao. Japokuwa wengine wamenufaika (pengine wewe ni mmoja wao), lakini bado kuna changamoto kadhaa.

Changamoto ya kwanza ni lazima mteja ajue akaunti yako, jambo ambalo si rahisi hasa kutokana na kuongezeka kwa watumiaji na watangazaji. Changamoto nyingine kubwa ni kutunza wale wateja uliopata au walau ambao wamevutiwa na huduma unazozitoa.

Kama una tovuti, unaweza kutumia huduma mbalimbali kutunza kumbukumbu za wateja wako, kuwasiliana nao kupitia barua pepe au simu za mkononi. Pia ni rahisi kuunganisha na tovuti nyingine zenye watumiaji wengi zaidi.

Hivyo basi, bila kujali aina au ukubwa wa biashara yako ni vema ukaanza kufikiria kutumia mtandao kuwafikia watu wengi zaidi. Hili litakuweka kwenye ushindani wa kimataifa, kama taifa tunatia aibu kwani nchi nyingine hasa majirani zetu Kenya wameitumia vyema fursa hii.

 

Neno la mwisho ni kuwa makini na watoa huduma za kutengeneza tovuti hizo. Ni vyema ukatafuta mtu unayemwamini kukushauri ufanyaje na kukupa njia sahihi. Kama wahenga wa kisasa wasemavyo ‘wapigaji wapo’ walau fika ofisini kwao, wajue vizuri na uzungumze na wateja wao wa zamani hata wawili watatu, jiridhishe kabla hujawapa kazi hiyo. Usilipie kitu ambacho hujakiona.

 

Mwandishi ni Gervas Mahimbi, ambaye ni Mkuu wa Idara ya Programming ya Smart Codes, akiwa msimamizi mkuu wa M-Paper.

+255716045525 / [email protected]

Twitter: @mahimbig

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles