25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Samia, Majaliwa watumia ndege za kukodi

magufulu akiwa na majaliwa na samia suluhuNA NORA DAMIAN, DAR ES SALAAM

MAKAMU wa Rais, Samia Suluhu Hassan na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wamelazimika kutumia ndege za kukodi baada ya ndege za Serikali kuharibika.

Wiki iliyopita, Samia alilazimika kutumia ndege ya kukodi alipofanya ziara ya kikazi ya siku mbili mkoani Tanga.

Pia Waziri Mkuu katika ziara zake mbalimbali amelazimika kutumia ndege za kukodi.

Wiki chache zilizopita, Majaliwa alitumia ndege ya kukodi kwenda mikoa ya Iringa na Mtwara na jana aliwasili mkoani Mwanza kwa ziara ya siku 14 katika mikoa ya Kanda ya Ziwa ambapo pia alitumia ndege ya kukodi.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ndege za Serikali (TGFA), Kapteni Kenan Mhaiki, alikiri ndege mbili za Serikali ambazo zimekuwa zikitumiwa na viongozi mara kwa mara kuwa ni mbovu.

Alizitaja ndege hizo ambazo kwa kawaida viongozi huzitumia katika shughuli za kawaida ndani ya nchi kuwa ni Fokker 50 na Fokker 28 (5H-CCM).

“Ndege zipo zinafanyiwa matengenezo, moja inahitaji matengenezo ya juu zaidi na nyingine inasubiri tu vipuri kutoka nje,” alisema Mhaiki.

Alisema hadi sasa ndege za Serikali zipo tatu, ikiwamo ya rais aina ya Gulfstream Aerospace (5H-One) ambayo anatumia sasa.

Alipotafutwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profsea Makame Mbarawa, alisema: “Suala hilo naweza kulizungumzia nikiwa Dar es Salam… niko kwenye mkutano nivumilieni.”

Mwanzoni mwa mwezi uliopita, Rais Dk. John Magufuli wakati akizungumza katika uzinduzi wa Mwaka wa Mahakama na Siku ya Sheria nchini, alisema kesi 442 zinazohusu wakwepa kodi endapo zitaamuliwa zitaiingizia Serikali Sh trilioni moja, fedha ambazo zinaweza kutatua ufumbuzi wa ndege za Serikali.

Alisema kiasi hicho cha fedha kinaweza kununua ndege aina ya Airbus takribani saba. Ndege moja inauzwa dola za Marekani milioni 90.1.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles