23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

‘RAILA KUPEPERUSHA BENDERA YA UPINZANI’

NAIROBI, KENYA


KINARA wa Chama cha ODM, Raila Odinga, anapewa nafasi kubwa zaidi kupeperusha bendera ya muungano wa upinzani wa Nasa.

Hiyo ni kwa mujibu wa mchambuzi mahiri wa siasa nchini hapa, Martin Andati.

Andati amedokeza hayo, huku tayari mpasuko ukionekana dhahiri ndani ya Nasa.

Jumanne wiki hii, Katibu Mkuu wa ODM, Seneta Maalumu, Agnes Zani na Katibu Mkuu wa Chama cha ANC, Godfrey Osotsi walitofautiana vikali.

Zani alisema kitendo cha Osotsi kusema hakuna ripoti ya namna vinara wa Nasa watakavyogawana nyadhifa ni upotoshi.

Seneta huyo ameonekana kukiri taarifa za awali kuwa Raila atakuwa mgombea urais na Kalonzo Musyoka wa Chama cha Wiper mgombea mwenza ni za ukweli.

ANC kinachoongozwa na Musalia Mudavadi, sasa kinadai ODM ni chama kinachohujumu utaratibu wa kumtafuta mgombea urais wa Nasa.

“Tumesikitishwa na Zani kukiri bayana ODM inahusika kusambaza propaganda na kuvujisha taarifa za siri kuhusu nyadhifa ndani ya Nasa na kuhatarisha kuisambaratisha,” alisema Osotsi.

Wakati sehemu ya hali ya mambo ndani ya Nasa ikiwa hivyo, Andati alisema mipangilio na mikakati ya Raila inadhihirisha yeye ndiye anayependelewa zaidi kuwakilisha umija huo kwenye Uchaguzi Mkuu wa Agosti 8.

"Mipangilio ya Raila kuendesha kampeni za kusaka kura katika Uchaguzi Mkuu, inaonyesha wazi yeye ndiye atakayepeperusha bendera ya Nasa," alisema Andati katika mahojiano.

Kwa mujibu wa Andati, Raila ni maarufu zaidi akilinganishwa na vinara wenza wa Nasa; Musyoka,  Mudavadi na Moses Wetang'ula wa Ford-Kenya.

"Raila mbali ya nguvu na ushawishi alionao, sasa ana umri wa miaka 72 na hawezi kukubali kumwachia yeyote apeperushe bendera ya Nasa. Mwaka wa 2022 atakuwa amefikisha miaka 77 na Katiba haitamruhusu kuwania urais tena.

"Kalonzo hana uwezo wa kufanya kampeni za urais kote nchini. Hakukusanya fedha za kutosha akiwa serikalini. Raila amejipanga hadi kifedha," alifichua Andati.

Kuhusu mkataba uliotiwa saini mwaka 2013 kati ya ODM na Wiper kuwa mwaka 2017  Raila atamuunga mkono Musyoka kuwania urais, Andati alisema mkataba huo hauna nguvu tena kwa sababu Nasa ni mrengo mpya.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles