Na MANENO SELANYIKA-DAR ES SALAAM
WAZIRI wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa amezitaka kampuni za mawasiliano nchini kuboresha huduma zao watumiaji wasihame kwenda mitandao mingine.
Profesa Mbarawa alitoa kauli hiyo Dar es Salaam jana wakati akizindua huduma mpya ya kuhama mtandao wa simu bila kubadili namba (MNP).
Alisema lengo la kuanzishwa huduma hiyo ni kuongeza ushindani na kuboresha huduma katika sekta ya mawasiliano ambako mtumiaji atahama kwenda mtandao mwingine kwa hiari yake.
“Kila kampuni imeshirikishwa katika mchakato wa kutoa maoni yake hivyo msiweke mizengwe na vikwazo kukwamisha mtumiaji ashindwe kuhamia mtandao autakao.
“Tunachotaka hapa ni kila Mtanzania popote alipo ndani ya nchi apate huduma nzuri na kwa gharama nafuu,” alisema Mbarawa.
Alisema Serikali itasimamia mfumo huo uendelee bila kukwama kwa kuzingatia hilo zitasimamiwa kanuni na sheria kwa wale watakaokiuka wataadhibiwa kwa mujibu wa sheria.
Waziri amewataka watumiaji wa mitandao kuzingatia sheria za matumizi ya mitandao ya jamii kuepuka matumizi mabaya yatakayokwamisha lengo.
Awali, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), James Kilaba, alisisitiza mambo 10 muhimu ambayo mtumiaji wa mfumo huo mpya anatakiwa kuzingatia.
Mwananchi atapata huduma hiyo sehemu yoyote katika maduka au kwenye kampuni yoyote ya mawasiliano nchini.
Alisema endapo mtumiaji atahama atakapohitaji kurudi katika mtandao wake wa awali itachukua siku 30 kukamilisha huduma hiyo.
Mwenyekiti wa Bodi ya TCRA, Dk. Johnes Kilimbe, alisema wao wataendelea kukemea matumizi mabaya ya mitandao ya jamii kwa kuwa wanaoathiriwa zaidi ni watoto ambao hupenda kuiga mambo wanayoyaona katika mitandao hiyo.