NEW YORK, MAREKANI
MKALI wa muziki nchini Marekani, Sean Combas ‘P. Diddy’, ameamua kubadili jina kwa mara nyingine na kujiita ‘Brother Love au Love’.
Mwishoni mwa wiki iliyopita msanii huyo alikuwa anasherehekea siku yake ya kuzaliwa, ambapo alikuwa anatimiza miaka 48 hivyo alitumia ukurasa wake wa Instagram na kuwaambia mashabiki wake kwamba ameamua kubadili jina badala ya kuitwa P. Diddy na sasa aitwe ‘Love au Brother Love’.
“Naomba niweke wazi, hii ni habari njema kwa mashabiki wangu, najua wapo ambao watachukia lakini haya ni maamuzi yangu, kuanzia sasa nimebadilisha jina naomba niitwe Love au Brother Love.
“Nimeamua kufanya hivyo kwa makusudi kwa kuwa mambo yangu mengi yamebadilika, hivyo nimeona bora nibadilishe na jina, mimi wa sasa si yule wa zamani, kuanzia sasa ukiniita Puffy, Diddy, Puffy Daddy au jina jingine lolote siwezi kuitika,” alisema msanii huyo.