24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

NYUMBA SALAMA INAVYOWAEPUSHA WATOTO NA UKEKETAJI

Na MALIMA  LUBASHA – SERENGETI


UKEKETAJI ni mila inayopigwa vita kutokana na athari zake  kwa watoto wa kike na wanawake. Licha yajitihada zilizopo za kuitokomeza mila hiyo, bado jamii nyingi za Kiafrika zinaiendeleza.

Nchini Tanzania makabila mengi  yanakeketa watoto wa kike, miongoni mwao ni Wakurya, Wamasai, Wagogo, Wanyaturu, Wanyiramba, Wakaguru.

Wataalamu wa magonjwa ya wanawake na watoto wanasema ukeketaji unapofanyika kuna sehemu kwenye uke huondolewa na kwa asili huwa inazovutika,  hivyo hukatwa kwa kutumia wembe au kisu.

Sehemu hiyo inapopona hubakiza makovu ambayo hayavutiki na hayapanuki hivyo husababisha maumivu makali.

Kwa kukosekana kwa mpanuko wakati mwanamke anapokaribia kujifungua madaktari hulazimika kumfanyia upasuaji.

Kama tunavyoendelea kuona na kusikia kupitia vyombo mbalimbali ukeketaji umeleta madhara makubwa, baadhi ya ndoa zimevunjika kutokana na wanaume kudai hawafurahishwi na wake zao waliofanyiwa ukeketaji wakati wa tendo la ndoa.

Wanawake na wasichana wanaoolewa na makabila yanayoendeleza ukeketaji  hujikuta wakifanyiwa kitendo hicho bila kuelewa pindi wanapojifungua, wakidai kwamba wanaondolewa uchafu na kurudisha maumbile ya mwanamke ili afanane na jamii hiyo.

Baadhi ya watu waliohojiwa na MTANZANIA wanasema mila na desturi za kabila la Kikurya wanapenda kukeketa watotowa kike ili kuwapunguzia hamu ya kufanya mapenzi na wanaume wengi.

Mratibu wa Nyumba Salama iliyopo katika mji wa Mugumu Wilaya ya Serengeti mkoani Mara, Rhobi Samwel ambaye ndiye mwanzilishi wa kituo  hicho anaelezea jinsi walivyoanzisha makazihayo.

Anasema alipeleka wazo hilo kwa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Mara, makao makuu yakiwa Musoma na kuahidi kumsaidia.

Samwel anasema mwaka 2011 Dayosisi hiyo ilipata fedha kutoka Rip Funding Evelop (RFE) ili kutoa elimu juu ya madhara ya ukatili na ukeketaji.

“Tulifanya kazi ya kuelimisha watu katika vijiji vya Ring’wani, Kenyana, Nyamitita, Magange, Kenyamonta, Nyagasense, Mesaga, Hekwe, Maburi, Gusuhi, Nyambureti na Monuna,” anasema Samwel.

Anasema baada ya elimu hiyo, Desemba mwaka 2012 kituo kilipata watoto 16 waliokimbilia hapo wakiomba hifadhi ili wasikeketwe.

Anasema huo ulikuwa ni mtihani kwa kituo kwani idadi ilikuwa kubwa hivyo hawakuwa na fedha za kumudu kuwahudumia.

Kwa kuwa alidhamiria kuwasaidia, aliomba fedha kwa wachungaji wa kanisa hilo pamoja na wadau wengine ili kutoa hifadhi kwa wasichana hao.

Anasema waliendelea na jitahada za kujenga kituo kikubwa ili kukidhi mahitaji.

Anasema mwaka 2014, walipokea watoto 136 ambao naowalikimbia kukeketwa, watoto 100 walifanikiwa kurudi kwa wazazi wao.

Anasema watoto 36 walibaki kituoni ambapo kati yao 26 walifundishwa kushona nguo na kupewa vyerehani.

“Watoto 10 waliokuwa wanasoma walipelekwa sekondari na wawili wapo kidato cha nne, wanane kidato cha tatu na wanaendelea vizuri na masomo,” anasema.

Anasema mwaka 2015 walipokea watoto 196 kutoka wilaya za Serengeti, Tarime, Butiama na Ngorongoro.

Desemba mwaka jana wakati wa msimu wa ukeketaji, walipokea watoto 241 kutoka wilaya za Serengeti, Tarime, Butiama, Rorya na Ngorongoro.

Anasema ili kituo kipate fedha za kujiendesha, wameanzisha kilimo cha bustani ili kupata chakula na kwamba hivi punde wanatarajia kuanzisha ufugaji wa kuku, mbuzi na ng’ombe wa maziwa.

“Sasa hivi tuna mashine za kutengeneza taulo za kike kwa ajili ya watoto hao na kuwagawia wanawake huko vijijini hasa wale wasio na uwezo.

Naye Mchungaji  wa Kanisa la Mennonite Tanzania (KMT), Cleofas Nyamataga anasema Mchungaji Nyamataga anasema jitihada hizo ziendelee ili kukomesha mila hiyo ambayo imesababisha vifo vya watoto wengi nchini.

Manga Johannes ni kijana wa kabila linaloendeleza ukeketaji, anampongeza Rhobi kwa kuanzisha Nyumba Salama na kuwakomboa watoto wa kike.

 

Sababu ya Rhobi kuanzisha Nyumba Salama

Mratibu huyo anaelezea historia yake jinsi alivyokacha kukeketwa.

Anasema; “Mimi ni msichana wa kabila Kikurya, baba yangu ni Mkurya na mama ni Mmasai, nikiwa shule ya msingi wazazi wangu walitaka nikeketwe lakini nilikataa.

“Nilitaka kutoroka lakini huko nilikotaka kukimbila sikuwa na ndugu yeyote.”

Anasema aliogopa mno kukeketwa kwa sababu rafiki yake waliyekuwa wakisoma naye darasa moja alifariki baada ya kukeketwa, ambapo alitokwa na damu nyingi mwili wake ukatupwa porini pamoja vitu alivyopewa zawadi ambavyo ni fedha na nguo, vyote vilitupwa ili kuondoa mkosi katika ukoo.

Kwa sababu hiyo aliamua kuanzisha kituo hicho ili kuwakomboa watoto wa kike dhidi ya ukeketaji.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles