25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

NONDO AHOJIWA URAIA IDARA YA UHAMIAJI

 Na MWANDISHI WETU-DAR ES SALAAM


MWENYEKITI wa Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP), Abdul Nondo, amehojiwa na Idara ya Uhamiaji Mkoa wa Dar es Salaam.

Taarifa hiyo ilitolewa jana na Mkurugenzi wa Idara ya Sheria TSNP, Paul Kisabo na kuthibitishwa na Ofisa Uhamiaji Mkoa wa Dar es Salaam (DCI), Crispin Ngonyani.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo,   kwa   wiki moja sasa Nondo alikuwa akihitajika na idara hiyo kwa mahojiano kuhusu   uraia wake.

Hata hivyo, pamoja na kuhitajika kwa kipindi hicho hakuweza kupatikana kutokana na changamoto kadhaa zilizokuwa zikimkabili.

“Jambo hilo tumelitimiza leo (jana). Baada ya kutoka Mahakama Kuu kwenye kesi yake ambayo imeahirishwa mpaka Aprili 11, 2018.

“Mnamo sa sita mchana tuliweza kumfikisha Abdul Nondo makao Makuu ya Ofisi za Uhamiaji mkoa (makao makuu ya wizara ya mambo ya ndani).

“Tulihoji alichoitiwa na anachotakiwa kujaza katika fomu aliyopatiwa. Jibu tuliambiwa wanataka kupata taarifa zake binafsi za wazazi wake, babu na bibi zake pande zote mbili (upande wa baba na upande wa mama).

“Pamoja na za ndugu zake, kwa sababu  ofisa uhamiaji mkoa alitamka kuwa sheria inawaruhusu kumuhoji mtu yeyote wanaemtilia shaka uraia wake na kuwa wana shaka na uraia wa Abdul Nondo, hivyo awathibitishie kuwa yeye ni raia wa Tanzania,” alisema Kisabo.

Alisema Nondo alijaza taarifa zile anazozifahamu na baada ya hatua hiyo ya mahojiano hayo na ofisa uhamiaji aliyekabidhiwa jukumu la kumhoji,     Aprili 20, 2018  Nondo anapaswa kupeleka cheti chake cha kuzaliwa, cheti cha kuzaliwa cha baba yake, mama yake, cha bibi na babu mzaa baba na mzaa mama.

Ofisa Uhamiaji Mkoa wa Dar es Salaam (DCI), Crispin Ngonyani, alisema ni kweli  taarifa hizo  zinazomhusu Nondo wanazihitaji.

Machi 21, mwaka huu Nondo, alifikishwa   katika Mahakama ya Wilaya ya Iringa na kusomewa mashitaka mawili ya kutoa taarifa za uongo mitandaoni na kudanganya kutekwa.

Nondo alifikishwa mahakamani hapo baada ya kusafirishwa usiku kutoka  Dar es Salaam alikokuwa akishikiliwa na polisi.

Alisomewa mashtaka hayo na Wakili wa Serikali, Abel Mwandalama mbele ya Hakimu Mkazi, John Mpitanjia.

Baada ya kusomewa mashtaka hayo, Wakili wa Nondo, Charles Luoga, alimuomba hakimu kumpatia dhamana mteja wake kwa kuwa makosa hayo yanadhaminika.

Hakimu alisema asingeweza kumpa dhamana kwa sababu watekaji bado wako mitaani na kwamba Nondo alikuwa anashikilia kwa usalama wake.

Hakimu  aliahirisha shauri hilo hadi Jumatatu Machi 26, mwaka huu  ambako Nondo aliweza kupewa dhamana.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles