23.6 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Mwanakijiji atolewa utumbo na Kiboko

Na WALTER MGULUCHUMA -KATAVI

MKAZI wa Kijiji cha Kasokola katika  Manispaa ya Mpanda mkoani Katavi, Nassor Omary, ameshambuliwa na Kiboko katika sehemu ya tumbo na mgongoni hadi utumbo wake kutoka nje.

Mwenyekiti wa  Kijiji  Hicho,   Domic  Fungameza  alisema  tukio  hilo la  kushambuliwa mtu  huyo lilitokea  juzi saa saba  mchana  katika  eneo la Chuo  cha  VETA  Mpanda .

Alieleza kuwa kabla ya tukio hilo mnyama  huyo  alijichanganya kwenye kundi la ng’ombe waliokuwa  machungajini.

“Ndipo  mchungaji  aliyekuwa na mifugo  hiyo alipokwenda kutoa taarifa kijijini hapo juu ya  kiboko huyo kujichanganya  na mifugo  ambayo  alikuwa akiichunga.

“Baada ya taarifa  hizo kuwa  zimefika  kijijini  hapo  kundi  kubwa la wanakijiji lilijikusanya na  kwenda  kwenye  eneo hilo  huku wakiwa na  silaha  za  jadi  huku  wengi wao  wakiwa na nia ya kwenda kumuua kiboko  huyo ili wapate kitoweo,”alisema .

Mwenyekiti huyo alisema  baada ya kufika kwenye eneo hilo walimkuta  kiboko  huyo akiwa bado kwenye kundi  la  ng’ombe ndipo walipoanza kumshambulia kwa kumpiga na mawe.

Alisema pamoja na mnyama huyo kukimbilia  kichakani wanakijiji waliendelea kumrushia  mawe na fimbo huku dhumuni lao kubwa   likiwa ni kutaka kumuua  ili  wapate kitoweo.

Alisema baada ya kuona anazidi kushambuliwa mnyama huyo alitoka mbio kwenye kichaka kwa lengo la kuwashambulia wanakijiji hao waliokuwa na silaha za jadi hatua iliyowafanya wanakijiji hao wakimbie.

Wakati wakiwa wanakimbia mnyama  huyo  alimshambulia  Omary sehemu za tumboni na pia alimjeruhi sehemu za mgongoni.

Pamoja  na  Omary  kupiga  mayowe ya kuomba msaada  kwa wanakijiji  wenzake   hakuna  aliweza kumpa  msaada na  badala yake waliendelea kukimbia hadi mnyama huyo alipoamua kutokomea kusikojulikana.

Mwenyekiti huyo alisema  baada ya  muda kupita wanakijiji  hao walirudi kwenye  eneo hilo na kumkuta mwenzao akiwa  amejeruhiwa  vibaya  hali  iliyowalazimu kumkimbiza Hospitali ya Mkoa wa Katavi kwa ajili ya matibabu ambapo amelazwa huku hali yake ikiwa mbaya.

Mmoja   wa  mashuhuda wa tukio hilo,  Kulwa   Sanane  alisema kiboko  huyo  alikuwa  hana  nia ya kumshambulia  mtu lakini alipata hasira baada ya kuona  anazidi kushambuliwa .

Askari wa maliasili walifika eneo hilo huku wakiwa na silaha na walianza kumsaka  kiboko huyo na walifanikiwa kumwona na kumpiga risasi hadi kufa.

Baada ya askari hao wa maliasili kumwua mnyama huyo, wananchi walifurika katika eneo hilo wakigombania kukata nyama ya kiboko huyo kwa ajili ya kitoweo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles