Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Hospitali ya Miracolo iliyopo Kata ya Segerea Wilaya ya Ilala inatarajia kutoa huduma za upimaji afya bure kwa magonjwa mbalimbali ikiwa ni maadhimisho ya miaka mitano tangu ilipoanzishwa.
Mratibu wa shughuli hiyo ambaye pia ni Daktari Bingwa wa Watoto wa Hospitali ya Miracolo, Anna Deogratias, amesema huduma hizo zitatolewa Mei 29 katika kituo cha daladala Segerea kuanzia saa 2 asubuhi.
Dk. Anna amesema baadhi ya magonjwa ambayo yatapimwa siku hiyo ni shinikizo la damu, kisukari, wingi wa damu, afya ya kinywa na meno, magonjwa nyemelezi na Ukimwi.
Aidha amesema kutakuwa na wataalam bingwa wa hospitali hiyo kwa ajili ya kutoa ushauri wa afya kwa wananchi watakaojitokeza kupatiwa matibabu.
“Kujua afya yako mapema ni muhimu kwa sababu unaweza kujiona mzima kumbe una matatizo, mwaka huu hospitali yetu inaadhimisha miaka mitano ya kutoa huduma kwa wananchi hivyo tumeamua kuadhimisha kwa kutoa matibabu bure kwa wakazi wa Jimbo la Segerea na maeneo ya jirani. Ndani ya miaka mitano Hospitali ya Miracolo tunajivunia kupata mafanikio makubwa ya utoaji huduma bora za afya,” amesema Dk. Anna.