23.6 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Micho: Nipo tayari kuifundisha Stars

Football - 2014 Chan Qualifier - Uganda Training - Mandela Stadium - Namboole - Kampala

NA MWANDISHI WETU, DAR ES SALAAM

KOCHA aliyeipeleka Uganda katika Fainali za Mataifa ya Afrika (Afcon) zitakazofanyika mwakani nchini Gabon, Milutin Sredojevic ‘Micho’, amesema yupo tayari kuchukua mikoba ya Charles Mkwasa ambaye anatarajia kumaliza mkataba wake Februari mwakani.

Micho aliyewahi kuwafundisha mabingwa wa soka Tanzania Bara, Yanga mwaka 2007, aliipa tiketi Uganda kushiriki michuano hiyo mikubwa Afrika baada ya miaka 38 pale walipoichapa Comoro bao 1-0.

Akizungumza na mtandao wa Soka360, Micho ameweka wazi kuwa yupo tayari kuifundisha Stars na kuipeleka Afcon kama alivyofanya kwa Uganda.

“Siogopi kuchukua kibarua cha kuinoa Taifa Stars na kuipeleka Afcon, kwanza ina wachezaji wazuri sana wanaohitaji kubadilishwa kutoka kwenye soka la kufurahisha jukwaa na kwenda katika ushindani,” alisema.

Kuhusu mkataba wake na Uganda The Cranes, Micho alisema ni kweli yupo katika mkataba na timu hiyo lakini hataona hatari kuuvunja kama atapewa ofa nzuri Tanzania.

“Nimebanwa na majukumu ya Uganda The Cranes, lakini hayanifanyi niache kusikiliza ofa nyingine, kama Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) wakinitaka nitawasikiliza na kurithi mikoba ya Mkwasa,” alisema.

“Kama Watanzania watanihitaji nitayatathmini kwa undani mapendekezo na maombi yao kwani naangalia mpango ulio bora zaidi.”

Hata hivyo, Micho ameshangazwa na madai ya Tanzania kuwa na changamoto ya wachezaji wanaoweza kuipeleka Afcon na kudai si kweli.
Alieleza hawezi kuhoji kwanini msururu mrefu wa makocha wa zamani wa Taifa Stars walishindwa kuipeleka Tanzania katika mashindano ya Afcon, lakini anaamini ndoto hiyo inawezekana.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles