Na JENNIFER ULLEMBO-DAR ES SALAAM
KOCHA Mkuu wa timu ya Taifa ya wanawake walio chini ya miaka 20 ‘Tanzanite’, Sebastian Nkoma, amesema mechi za kirafiki zinatosha kukiwezesha kikosi hicho kuibuka na ushindi mnono dhidi ya Nigeria.
Tanzanite inatarajiwa kuvaana na Nigeria katika mchezo wa kutafuta kufuzu Fainali za Kombe la Dunia dhidi ya Nigeria, uliopangwa kufanyika kati ya Septemba 15, 16 au 17, jijini Lagos.
Akizungumza na MTANZANIA jana, Nkoma alisema ana imani kikosi chake kikipata mechi za majaribio kabla ya mchezo huo kitaweza kujiimarisha zaidi.
“Hapa tukipata mechi za majaribio kila kitu kitakuwa sawa, wachezaji wanaendelea kujifua kama kawaida ili kuhakikisha katika mchezo huo muhimu tunaibuka na ushindi,” alisema Nkoma.
Alisema kuwa, wachezaji wake wamedhamiria kufanya kweli na kupata nafasi ya kucheza fainali hizo baada ya Tanzania kushindwa kufanya vizuri katika ramani ya soka upande wa wanawake kwa muda mrefu.
Timu hiyo inaendelea na kambi katika hosteli za Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), huku ikifanya mazoezi katika Uwanja wa Karume.