24.7 C
Dar es Salaam
Tuesday, March 19, 2024

Contact us: [email protected]

Makala| Rehema: Mwanangu alifariki sababu ya utoto wangu-2

Na Faraja Masinde, Mtanzania Digital

Ripoti ya matokeo ya utafiti unaoitwa ‘Ndoa za utotoni Tanzania’ iliyotolewa Mchi 2, 2017 inasema wasichana wanaoingia katika ndoa mapema pia hupata ujauzito mapema, hali ambayo huwaweka katika hatari zaidi wakati wa ujauzito na kujifungua

“Kwa mfano, wakinamama kati ya umri wa miaka 15 na 19 wanao uwezekano wa kufariki mara mibili zaidi ikilinganishwa na wakinamama ambao wenye umri kati ya miaka 20 na 24,” inasomeka sehemu ya ripoti hiyo iliyotolewa na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jami, Jinsia, Wazee na Watoto kwa kushirikiana na taasisi kadhaa zikiwamo Plan, CDF, Forward na UNFPA…endelea sehemu ya pili.

Maisha yake ya sasa

Akizungumzia maisha yake ya sasa Rehema anasema kuwa, ni kama anasogeza tu siku ziende kwani amani na furaha ya ndoa ndani ya nyumba yao ilishatoweka siku nyingi.

“Hapa mimi nipo tu kwa ajili ya watoto wangu wakue basi niondoke kwani ndoa yetu haina amani tena, kwani mume wangu hata kwenye shughuli zake za biashara ameniambia sitakiwi kushiriki, lakini mimi naenda sababu nahitaji kupata mahitaji yangu mbali na fedha anayoacha kwa ajili ya chakula.

“Kuna wakati ananigombeza sana hadi natamani nichukue vitu vyangu niondoke, lakini ananiambia kuwa nikifanya hivyo maisha yangu yatakuwa hatarini na sitapata mwanaume wa kunioa tena, hivyo navumilia tu na kumuachia Mungu, lakini ukweli ni kwamba maelewano ndani ya nyumba hakuna,” anasema Rehema.

Rehema anaongeza kuwa kuna wakati aliwahi kumfumania mumewe huyo akiwa na mwanamke mwingine lakini aliporudi nyumbani badala ya kumwomba msamaha alimpiga akimwambia kama anataka basi amzalie mtoto wa kiume.

“Mbali nakujishughulisha kwenye biashara zake, lakini muda wangu mwingi umekuwa ukiishia kanisani kwani kwa ajili ya kumuomba Mungu abadilishe hii hali,” anasema Rehema.

Ripoti ya matokeo ya utafiti unaoitwa ‘Ndoa za utotoni Tanzania’ iliyotolewa Mchi 2, 2017 inasema wasichana wengi walioolewa katika umri mdogo hupata vipigo kutoka kwa waume zao kiasi cha wengine kupoteza maisha. 

“Asilimia 40 ya waliohojiwa waliripoti kuwa walitukanwa, wakati asilimia 39 waliripoti kupigwa au kupigwa makofi, na asilimia 35 kutelekezwa au kufukuzwa,” inasomeka sehemu ya ripoti hiyo.

October 29, 2014 Shirika la kimataifa linalofuatilia haki za binadamu la Human Raights Watch lilitoa ripoti madharayanayowapata wasichana nchini Tanzania kutokana na ndoa za utotoni  likisema wengi wanaathirika kwa kukosa elimu, huku wakibainisha kwamba katika baadhi ya jamii wapo mabinti waliolazimiwa kuolewa wakiwa na umri hadi wa miaka saba.

Ripoti hiyo inaoitwa “‘Hakuna Jinsi’: Ndoa za Utotoni na Ukiukwaji wa Haki za Binadamu ndani ya Tanzania,” Human Rights Watch wanasema wasichana wadogo wanaoingia kwenye ndoa pia huwa hatarini kufanyiwa unyanyasaji na ukatili – ikiwemo kubakwa ndani ya ndoa na hatari ya afya ya uzazi.  

Takwimu za mwaka 2015/ 2016 kwa wanawake wanaofanyiwa ukatili na wenza wao zinaonyesha kwamba mikoa kinara yenye kiwango cha juu kwa wanawake kufanyiwa ukatili nchini Tanzania ni pamoja na Mara na Shinyanga ambazo zote zina asilimia 78 huku kiwango cha nchini kikiwa ni katika mikoa ya Kaskazini Pemba asilimia 8 na Kusini Pemba asilimia 9.

Kadhalika Ripoti ya Shirika la Afya Duniani(WHO) -ya mwaka gani? inahitaja Tanzania kama nchi ambayo unyanyasaji wa wanawake wanaofanyiwa na wenza wao ni jambo la kawaida ikilinganisha na mataifa mengine zilizofanyiwa utafiti kama huo.

Aidha, WHO inaiweka Tanzania katika kundi la nchi 12 zenye hatari zaidi ya unyanyasaji wa wanawake katika ukanda wa Afrika.

Mgongano wa kisheria

Mara kadhaa wataalamu wa sheria wamebainisha kuwapo mgongano wa kisheria katika kufafanua tafsiri ya Mtoto kwa muktadha wa ndoa.

Katika tamko la siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia mwaka 2022 Wanaharakati wa Haki za Binadamu walbainisha kuwa Sheria ya Ndoa ya Tanzania inapingana na Sheria nyingine ambazo zinafafanua tafsiri ya mtoto. 

“Wakati Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009, inamwelezea mtoto kama mtu mwenye umri chini ya miaka 18, Sheria ya Ndoa bado inamruhusu mtoto mwenye umri wa miaka 15 kuolewa kwa ruhusa ya wazazi,”inaeleza sehemu ya tamko hilo na kuongeza:

“Tafsiri ya mtoto chini ya Sheria ya Mtoto haijabatilisha kifungu cha 13 ya Sheria ya Ndoa ambacho kinaweka umri wa chini wa ndoa kuwa miaka 15 kwa wasichana na 18 kwa wavulana”. 

Itakumbukwa kuwa mwaka 2019, Mahakama ya Rufaa ya Tanzania ilithibitisha uamuzi wa Mahakama Kuu katika kesi ya Mkurugenzi wa Taasii ya Msichana Initiative, Rebeca Gyumi dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na kuitaka Serikali kuvifanyia marekebisho.

Katika uamuzi wake Mahakama ya Rufaa ilisema vifungu hivyo ambavyo vinaruhusu mtoto kuolewa na umri wa miaka 15 kwa idhini ya wazazi na 14 kwa ruhusa ya mahakama ni vya kibaguzi dhidi ya mtoto wa kike na ni kinyume na Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania. 

Kadhalika ilielekeza virekebishwe ndani ya miezi 12. Hata hivyo Sheria ya ndoa, haijabadilishwa mpaka sasa na mara kadhaa Serikali licha ya kukiri kushindwa kesi imekuwa ikisema inashindwa kuvifanyia marekebisho kutokana na unyeti wa kitamaduni na wa kidini juu ya jambo hilo.

Hata hivyo Jaji Mstaafu wa Mahakama Kuu, Robert Makaramba alisema kwa kuzingatia uamuzi uliofanywa na Mahakama ya Rufani kuhusu suala hilo, mtu yeyote anayeingia katika uhusiano wa kindoa na mtu mwenye umri chini ya miaka 18 anatenda kosa la jinai kwa mujibu wa Sheria.

“Hata kama Sheria ya Ndoa haijabadilishwa, lakini katika muktadha wa mamlaka ya mahakama, uamuzi wa Mahakama ya Rufani ni sheria tayari. Bunge linaweza kurekebisha mambo mengine katika sheria husika, lakini suala la umri ambalo limetolewa uamuzi na Mahakama ya Juu kabisa katika nchi yetu, haliwezi kubadilishwa nje ya mfumo wa kimahakama,”alisema Jaji Makaramba katika hafla ya uzinduzi wa machapisho ya Baraza la Habari Tanzania (MCT).

Kwa upande mwingine ya ndoa pia inakinzana na Sheria ya Elimu nchini Tanzania ya mwaka 1978 kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2016 ambayo inapiga marufuku ndoa za wanafunzi, huku ikiweka adhabu kali ya hadi kifungo cha miaka 30 jela kwa mtu atakayetiwa hatiani kwa kosa la kuingia kwenye ndoa na mwanafunzi.

Nani anawajibika?

Kumekua na mapendekezo mengo juu ya nani anayepaswa kuwajibik katika matukio yanayomkandamiza mtoto wa kike nchini na moja kubwa lilikuwa ni lile la kutaka wasichana wanaopata ujauzito warejee shule baada ya kujifungua, ambalo tayari serikali imekubaliana nalo.

Hata hivyo wadau wa masuala ya haki za binadamu pamoja na kupongeza uamuzi wa serikali katika eneo hilo wamekuwa wakisisitiza kwamba itungwe sheria na kanuni za kuweka utaratibu rasmi ili kuupa nguvu ya kiutekelezaji.

Ripoti inayoitwa “Hakuna Jinsi’: Ndoa za Utotoni na Ukiukwaji wa Haki za Binadamu ndani ya Tanzania,” iliyotolewa Oktoba 29, 2014 na Shirika la Human Rights Watch (HRW) imeorodhesha hatua nyingi zinazopaswa kuchukuliwa na wadau mbalimbali katika muktadha mzima wa kupamba na ndoa za utotoni.

Miongoni mwa mapendekezo hayo ni kumwomba Rais wa Rais wa Tanzania kutoa kauli za kulaani hadharani ukatili dhidi ya wanawake na watoto wanaokataa ndoa za utotoni, za mapema, na za kulazimishwa na aunge mkono hadharani kuwekwa kwa mfumo wa umri mdogo wa kuoa au kuolewa kwa wavulana na wasichana unaolingana na unaotambulika kimataifa kuwa miaka 18. 

HRW wanasema jukumu jingine ni la Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ambayo inapasa kurekebisha Sera ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ili ijumuishe kifungu ambacho kinaruhusu wanafunzi walioolewa na wenye mimba kuendelea na elimu yao na kuhakikisha wasichana wanaoandishwa shule wanahitimu elimu yao.

“Wizara ya Elimu ianzishe mchakato wa kutambulisha mtaala wa elimu ya afya ya uzazi kwenye shule za msingi na sekondari ambao unalingana na viwango vya kimataifa vya haki ya binadamu,” inasomeka sehemu ya mapendekezo hayo.

Kwa Wizara ya Katiba na Sheria, HRW wanapendekeza kwamba ifanyie kazi na uchambuzi wa kina wa kuboresha sheria ya ndoa na kutaja wazi kwamba umri mdogo wa kuoa au kuolewa kwa wavulana na wasichana ni miaka 18. 

Mtaalamu wa saikolojia, Christian Bwaya anaeleza kuwa mara nyingi andoa ambazo mwanamke huaolewa na mtu mwenye umri sawa na wa baba yake au babu yake huwa hazina haiba kwani hazitosi fursa ya kusikilizana kwa upande wa binti.

“Aina hii ya ndoa un akuta haina furaha hata kidogo kwani muda mwingi binti anakuwa ni mhanga wa maamuzi yanayofanywa na mume wake, na hapa mara nyingi hata binti huyu akitoa ushauri ni ngumu sana kusikilizwa.

“Hatari zaidi ipo kwa zile ndoa ambazo binti alikutanishwa tu na mwanaume huyu bila kumuona au kumjua hapo awali, hivyo wazazi wamekuwa nisehemu ya kuuminya uhuru wa mabinti kufanya maamuzi na kutimiza ndoto zao na hivyo kuchochea ndoa za utotoni,” anasema Bwaya.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
584,000SubscribersSubscribe

Latest Articles