24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Mabango ya ubaguzi CCM yazua tafrani

bangoNa Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimelaani ujumbe wenye maudhui ya ubaguzi ulioandikwa kwenye bango lililobebwa na mmoja wa wananchi waliojitokeza katika maadhimisho ya sherehe za miaka 52 ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Taarifa iliyotolewa jana kwa vyombo vya habari na Mkuu wa Mawasiliano na Umma wa CCM, Daniel Chongolo, ilieleza kwamba chama hicho kimesikitishwa na ujumbe huo na kuwaomba radhi Watanzania.

“Tumesikitishwa sana na ujumbe huo uliokuwa katika bango hilo, CCM kinaomba radhi kwa ujumbe huo, kinapinga na kinakemea kabisa fikra, hisia na mitazamo yoyote yenye maudhui ya kibaguzi.

“Ujumbe huo si tu kuwa una maudhui ya kibaguzi, bali pia unaenda kinyume kabisa na falsafa na shabaha ya waasisi wa Mapinduzi hayo matukufu ya mwaka 1964 na unapingana na misingi na itikadi ya CCM inayohimiza umoja na mshikamano wa kitaifa,” alisema Chongolo katika taarifa yake.

Hatua hiyo ya CCM imekuja baada ya wananchi mbalimbali kupitia mitandao ya kijamii kulaani bango hilo ambalo walionya kuwa halina nia njema na mshikamano wa Taifa.

Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe, alisema siasa za namna hiyo hazifai na zinapaswa kulaaniwa na kila mpinga ubaguzi nchini.

“Nitashangaa sana kama wakubwa CCM hamtaomba radhi kwa siasa hizi mbaya kabisa ‘What will be the stop’,” alisema Zitto ambaye pia ni mbunge wa Kigoma Mjini.

Kutokana na tafrani hiyo ya ubaguzi, nacho Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimelaani kile walichodai chembechembe za ubaguzi wa aina yoyote visiwani humo.

Taarifa iliyotolewa na Mkuu wa Idara ya Mawasialino wa chama hicho, Tumaini Makene, ilieleza kwamba Chadema kwa kusimamia misingi ya utaifa hasa haki, uadilifu, utu, umoja na uzalendo haiko tayari kuona Taifa linafikishwa huko na hata kuhatarisha maisha ya jamii nzima ya Watanzania.

“Chadema tunalaani na kupinga kwa nguvu zote mipango, mikakati, tabia na chembechembe za ubaguzi wa aina yoyote, ukiwemo huu wa kisiasa ambao sasa unaanza kusakafiwa kwa ubaguzi wa rangi.

“Kwa sababu tunaamini wanaobeba ajenda hii hawataishia hapo bali watazidi kutugawa Watanzania pia kwa ukanda, ukabila, udini kama wamekuwa wakijaribu kuchochea,” alisema Makene.

Kutokana na kauli hiyo, alisema wanamkumbusha Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Ernest Mangu, kuhakikisha anawachukulia hatua wale wanaoeneza chuki na hatari ya kuvurugika kwa amani kwa ujumbe wa kibaguzi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles