23.6 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

LISSU AHOJIWA POLISI KUPOTEA KWA BEN SAANANE

MBUNGE wa Singida Mashariki, Tundu Lissu
MBUNGE wa Singida Mashariki, Tundu Lissu

Na TUNU NASSOR-DAR ES SALAAM

MBUNGE wa Singida Mashariki, Tundu Lissu, amehojiwa na Jeshi la Polisi kutokana na kauli zake kuhusu tukio la kupotea kwa Ben Saanane ambaye ni msaidizi wa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe.

Lissu alijisalimisha Kituo Kikuu cha Polisi, Dar es Salaam jana saa 3:40 asubuhi huku akiwa na wakilishi wake baada ya kutakiwa kufanya hivyo na jeshi hilo.

Akizungumza na MTANZANIA baada ya mahojiano hayo, Wakili wa Lissu, Frederick Kihwelo, alisema mteja wake aliitwa na jeshi hilo kwa mahojiano maalumu.

Alisema baada ya wito huo, yeye na mteja wake waliwasili katika kituo hicho, ambako alihojiwa na kuruhusiwa kuondoka saa 10 alasiri.

“Ni kweli Lissu aliitwa na Jeshi hilo. Amechukuliwa maelezo kutokana na kauli alizozitoa katika mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika Desemba 14, mwaka huu, alipozungumzia kupotea kwa Msaidizi wa Mwenyekiti wa Chadema, Ben Saanane,” alisema Kihwelo.

Alisema Lissu alihojiwa na maofisa wa juu wa Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam na baadaye kuitwa Ofisi ya Upelelezi wa Mkoa (RCO) ambako alihojiwa tena.

Kihwelo alisema mteja wake alihojiwa kama anakifahamu kikosi kazi alichokizungumzia katika mkutano wake huo.

“Lissu amejibu kuwa anakifahamu kikosi kazi hicho kwa kusikia baadhi ya watu wanapotafuta ndugu zao huambiwa kuwa wanashikiliwa na kikosi hicho kinachojumuisha Usalama wa Taifa, Polisi na wanajeshi,” alisema.

Kihwelo aliongeza kuwa Lissu alihojiwa pia kwanini kila anapotamka jina la Rais humwita Mtukufu sana.

“Katika mahojiano hayo, hoja zao zilijikita katika mambo manne aliyoyasema Lissu katika mkutano wake, ambayo alilitaka Jeshi la Polisi kusema kama linamshikilia Saanane, kama yuko nje ya nchi alipitia njia gani kuondoka nchini, mawasiliano ya mwisho aliyoongea nayo kabla ya kupotea na kwanini maiti saba zilizookotwa Mto Ruvu zilizikwa bila kufanyiwa uchunguzi,” alisema Kihwelo.

Saanane alipotea ghafla katika mazingira ya kutatanisha takribani mwezi mmoja sasa na hajulikani alipo jambo ambalo limezua hofu kama yu hai ama la.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles