27.2 C
Dar es Salaam
Thursday, May 2, 2024

Contact us: [email protected]

KENYATTA : SGR KUKAMILISHA UCHUMI VIWANDA KENYA

Na  Shermarx Ngahemera


RAIS Uhuru Kenyatta wiki iliyopita alizindua reli ya mfumo wa kisasa wa SGR kwa safari za Mombasa hadi Nairobi utakaogharimu zaidi ya dola bilioni 3.3 reli itakapomalizika kwa kilomita 1062 (maili 660).

Awamu ya kwanza iliyokamilika ni maili 378  ikiwa ni kutoka Mombasa hadi Nairobi iliyopangwa kuenda hadi Malaba mpakani na nchi ya Uganda. 

Akizungumza kwenye uzinduzi wa  kumalizika awamu ya kwanza Rais Kenyatta alisema kuwa ujenzi wa reli hiyo ni hatua muhimu iliyofanywa  na serikali ili kuwezesha uwekezaji katika eneo hilo  muhimu kwa uchumi wa Kenya na azma  yake ya kuwa nchi ya uchumi wa viwanda.

Alisema kazi iliyofanyika ni kubwa na nzuri na aliwapongeza Wachina kwa utendaji kazi wao  ambao ni mzuri kuigwa na kunaliza kwa wakati na kutegemea muendelezo wake  utakuwa mzuri kwenda Kisumu na Malaba mpakani na Uganda.

Alisema reli hiyo itapunguza gharama za usafirishaji kwa kiasi kikubwa na kuongeza  ushindani wa taifa la Kenya kibiashara na hivyo kuvutia  watalii na wawekezaji ambao wataongeza ajira nchini humo.

Akitoa mfano ni kuwa kontena  moja toka Mombasa ambalo lilikuwa linagharimu shilingi 90,000/- kulisafirisha toka Mombasa  hadi Nairobi sasa litagharimu shilingi 50,000/-,  karibu nusu ya bei. Reli pia imepunguza muda wa kusafiri kutoka saa 10 hadi 4.

Huu ni mradi mkubwa wa miundo mbinu kufanywa na  Kenya toka ipate uhuru na umepangwa kuondoa reli ya mita iliyojengwa na Waingereza miaka zaidi ya 100 iliyopita iliyokuwa inajulikana kimasihara kama ‘Reli ya Wendawazimu’ ambayo iliunganisha Mombasa na Ziwa Victoria.

Mwenyekiti wa Shirika la Reli la Kenya  (KRC)Jenerali Profesa Jeremiah Kianga anasema pongezi ziende kwa Rais Kenyatta kwa juhudi zake binafsi ambapo aliweza kuhudhuria vikao vya Bodi vyote vilivyokuwa vinajadili mwenendo wa mradi huo na kufanya maamuzi ambayo yaliwezesha mradi kumalizika  mapema zaidi ya vile ilivyopangwa.

Alisema Rais aliingilia kati mara nyingi pale kulikoonekana kukwamisha  mradi na kuwezesha masuala ya ardhi, mbuga za wanyama na masuala mengine nyeti ya mradi.

Alisema ujenzi uliweza kuajiri watu 45,000 na kampuni 1800 zilitumika kutoa huduma mbalimbali kwa wajenzi kampuni ya China Railway Builders Contractors (CRJBC).

Uganda inategemea kuanza ujenzi wa sehemu ya reli nchini mwake kutoka Kampala   hadi Malaba kuanzia mwishoni mwa mwaka huu kutokana na mkopo kutoka benki hiyo hiyo ya Import Export China.

China imeweza vilevile kutoa fedha za ujenzi wa reli ya kisasa kwa Ethiopia kwa kuingunisha na Bandari ya Djibouti katika Ghuba ya Aden katika mkakati mzima wa mradi wa China wa ‘Mkanda na Njia’ (Belt and Route Initiative)

Habari toka China zinasema kuwa nchi hiyo ina mipango ya kuhamisha ajira za gharama ya chini za uzalishaji viwandani milioni 100 kwenda nje ya China na Kenya imelengwa kupata kipaumbele.

Awamu ya Pili yakwama

Mkurugenzi wa Kampuni ya Ujenzi CRJBC Lu Xan amefurahi kushiriki katika ujenzi huo kuonesha ujuzi na uzoefu wa nchi yake wa zaidi ya miaka 70 katika ujenzi wa reli katika sehemu mbalimbali nchini humo na duniani katika miradi mikubwa  mbalimbali.

Lakini changamoto zimeanza kujitokeza ambapo  awamu ya pili inaonekana kugota baada ya mahakama kuzuia ujenzi wa  SGR  kutoka Nairobi kwenda Malaba kutokana reli hiyo kupita katikati ya Mbuga Wanyama ya Nairobi. Wanamazingira wanadai ujenzi utasababisha madhila mengi kwa wanyama pori na hivyo kudai mahakamani na Mahakama imetoazuio la muda,

Kwa vigezo vyote reli hiyo ni ya mtindo wa kisasa kwa mizigo na abiria na ilitegemewa kwisha Mwishoni mwa mwaka lakini iliharakishwa ili kuongeza tija kwa serikali iliyoko madarakani kwa mwaka huu wa uchanguzi hapo Agosti.

Taarifa toka jijini Harbin mji mkuu wa jimbo la Heilojiang, China zinasema kuwa treni 10  na mabehewa yake zimeshawekwa melini kuja Kenya kutumika katika reli hiyo mpya.

“X2K ni mabehewa ya pande mbili na inabeba mzigo wa tani 78 au kubeba makasha  (containers) 4 ya futi 20 ambazo zitahimili shughuli iliyokusudiwa,” imeripoti China Daily.

Wasiwasi mkubwa wa mradi mzima ni utunzaji ; uoga wa kutelekezwa  kama  ilivyofanyiwa  reli iliyopo na hofu ya uendeshaji na kukosekana matengenezo madhubuti ya reli hiyo baada ya kukabidhiwa  ingawa Wachina wataiendesha kwa miaka sita ya mwanzo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles