25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

KABILA ASHUTUMIWA NA MDOGO WAKE, ATAKIWA ANG’OKE

NAIROBI, KENYA


KAKA wa kambo wa Rais Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), amejiunga na wale wanaoendesha kampeni ya kumshinikiza aondoke madarakani, akimtuhumu kwa kukaa nje ya muda unaomruhusu kikatiba.

Emmanuel Masirika Kabila (32), mtoto wa marehemu Laurent Desire Kabila, anasema kaka yake Rais Kabila anapaswa kuondoka madarakani na kuruhusu nchi iendeshe sensa ya kitaifa, ambayo ilifanyika mara ya mwisho mwaka 1984.

Pia ametaka kuondolewa kwa Mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi (CENI), Corneille Nangaa, akimtuhumu kuwa sehemu ya mipango ya Kabila kubaki madarakani.

Emmanuel aliyezaliwa Ankoro katika Jimbo la Katanga mwaka 1985, mama yake akiwa Victorine Hakiza Masirika kutoka Kivu, kusini mashariki mwa Congo, alikuwa mmoja wa wake kadhaa wa marehemu Kabila.

Marehemu Kabila ana watoto 25 waliotokana na wanawake tofauti kwa vile hakuishi eneo moja ndani ya DRC na nchini Tanzania akikwepa mikono ya aliyekuwa Rais Mobutu Sese Seko.

Mara baada ya Emmanuel kuzaliwa, baba yake alikimbilia Tanzania na mama na mtoto wakaungana ugenini mwaka mmoja baadaye.

Masirika aliuawa mwaka 1994 na askari wa Mobutu wakati akiwa kwenye operesheni ya kijasusi huko Ankoro.

Akizungumza na gazeti la The East African mjini hapa, Emmanuel alisema aliikimbia DRC Desemba 2011 kutokana na mateso kutoka vikosi vya usalama na tisho la maisha yake.

“Ugomvi wetu unatokana na kumwomba Rais Kabila kuanzisha uchunguzi wa mauaji ya baba yangu, kuwaachia huru waliokamatwa kimakosa na kurudisha urithi na utajiri wa familia yetu,” alisema.

Aliutuhumu utawala wa kaka yake kwa kuwatesa baadhi ya wanafamilia kufuatia kuuawa kwa baba yao Kabila mwaka 2001.

“Tunatafuta sababu za kuuawa kwa shangazi yangu, Esperance Mukalayi mwaka 2005, na dada yangu Aime Mulengela Kabila mwaka 2008,” alisema Emmanuel, ambaye anaishi uhamishoni Afrika Kusini.

Katika masuala ya kisiasa, Emmanuel, ambaye alikataa kuthibitisha au kukana uvumi kuwa amepanga kuwania urais katika uchaguzi wa Desemba 23, alikuwa na shaka iwapo kweli kaka yake ataondoka madarakani baada ya uchaguzi.

Alisema Rais Kabila —ambaye mihula yake ya kikatiba iliishia mwaka 2016—ana wasiwasi kuwa akiondoka madarakani bila kinga anaweza kushtakiwa kwa ukiukaji wa haki za binadamu na mauaji ya wanaharakati wanaotaka aondoke.

Kabila hivi karibuni aliliamuru Bunge kujadili hadhi ya marais wa zamani, ikiwamo kinga ya kutoshitakiwa na stahili zao.

Lakini Emmanuel, ambaye pia ni mwenyekiti wa Kamati ya Ukombozi wa Watu wa Kongo anataka Rais Kabila ajibu tuhuma za kupotea kwa wanafamilia tangu kuuawa kwa baba yao mwaka 2001.

 

 

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles