24.8 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

JINSI YA KUMFUNDISHA MTOTO KUWA MUUNGWANA

Na CHRISTIAN BWAYA,

UMEWAHI kumpa mtu kitu anachokihitaji lakini haoni sababu ya kusema; “ahsante?” Mtu anakukosea na hawezi kusema; “samahani” au “nisamehe?” Wapo wengine hata ufanye vizuri namna gani kusema, “hongera umefanya vizuri” ni kama adhabu na kujishushia hadhi. Hizi ni baadhi ya tabia zinazoweza kuonesha namna mtu asivyo muungwana na zinaweza kumpunguzia thamani yake mbele ya jamii.

Uungwana ni namna mtu anavyoweza kujali hisia za wengine. Kuelewa mwenzako anataka nini, anajisikiaje unaposema maneno fulani, anachukuliaje unapomfanyia mambo fulani na mengineyo kama hayo. 

Kuna msemo uliozoeleka kuwa tabia za watoto ni sura ya walivyo wazazi wao. Tafsiri ya msemo huu ni kuwa kile anachokifanya mtu, kwa kiasi kikubwa, kinatokana na yale anayojifunza kwa wazazi wake. Ndio kusema uungwana anaojifunza mwanao unakutegemea namna wewe mzazi unavyojiweka mbele yao, kwa maneno, kwa matendo na hata kwa tabia.

Hebu tutazame mambo manne muhimu unayoweza kuyawekea mkazo pindi unapomfundisha mwanao uungwana.

Kushukuru

Kushukuru ni kurudisha fadhila unazotendewa na wengine. Kwa mfano; unapopewa huduma nzuri dukani ni uungwana kushukuru hata kama ni kweli umeilipia huduma hiyo. Tabia ya kushukuru tunajifunza na hatuzaliwi nayo. Ikiwa unataka mwanao awe mtu mwenye uwezo wa kutambua mema anayotendewa na wengine, ni muhimu uitilie mkazo tabia hata ikibidi kwa kuweka mazingira ya kulazimisha.

Mfano, jenga utaratibu wa kudumu unaomlazimisha kila aliyeshiriki chakula hapo nyumbani kusema ahsante. Utamaduni huu wa kushukuru unawezekana ikiwa wewe mwenyewe utaanza kuonesha mfano. Mshukuru mwezi wako mbele ya watoto wako. Washukuru watoto wako wanapokutendea kile unachokipenda. Kadhalika, wakumbushe kushukuru kila wakati.

Kupongeza

Mtu mwingine anapofanya jambo zuri ni uungwana kumpongeza. Pongezi humfanya anayepongezwa kujisikia vizuri. Mfundishe mtoto kutambua mazuri yanayofanywa na wengine na kutamka maneno sahihi.

Kwa kutoa pongezi, Tafuta kutambua jitihada zinazooneshwa na wanafamilia na toa pongezi kwa moyo wa dhati. Unaweza kuwapongeza watoto kwa jitihada wanazoonesha katika masomo. Mpongeze mke/mume wako anapofanya vizuri mbele ya watoto na bila aibu. Wahimize wanao kupongezana ili kujenga tabia ya kupongeza wengine.

Kuomba msamaha na kusamehe

Kukosea ni sehemu ya mapungufu yetu binadamu. Lakini si kila mtu anaweza kuwa tayari kuomba msamaha hata pale anapojua amekosea. Wanafikiri kuomba msamaha ni kujishushia hadhi zao. Ikiwa unataka mwanao awe na tabia ya kuomba msamaha na kuwasamehe wanaomkosea unawajibika kumfundisha.

Onesha mfano wewe mwenyewe kwa kuomba msamaha mbele ya wanao. Mwombe msamaha mke/mume wako hata kwa mambo madogo unayomkosea. Waombe msamaha wanao unapogundua umefanya kosa. Walazimishe na wao kuombana msamaha wanajikuta kwenye makosa. Ukweli ni kwamba mtoto anapokuwa na tabia ya kuomba msamaha, ni rahisi kusamehe wengine pale anapokosewa.

Kuwajali wengine

Kuthamini wengine ni kujiona kuwa huwezi kuwa bora kuliko watu wengine. Hiyo haina maana kuwa hujiamini. Hapana! Kimsingi unapojiamini ni rahisi kuwathamini wengine. Unao wajibu wa kumfundisha mwanao tabia ya kuwathamini watu wengine.

Anza kwa kuwaonesha watoto wako vile unavyowathamini. Wanapoumia, onesha kujali na wape pole bila kuchelewa. Watakapojua unawajali, hawatapata tabu kuwajali wengine. Wakumbushe wajibu wao wa kutoa pole kwa wenye shida na wanaoumia. Kwa kufanya hivyo utajenga mazoea mazuri ya kuwajali wengine.

Blogu: http://bwaya.blogspot.com , Simu: 0754 870 815

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles