23.3 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

GGML, NEEC waanzisha mafunzo kwa wafanyabiashara

NA MWANDISHI WETU

KATIKA jitihada za kuwapatia maarifa na ujuzi wajasiriamali mkoani Geita juu ya mchakato wa manunuzi yanayofanywa na Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML), kampuni hiyo imefadhili mafunzo maalum yanayoratibiwa na Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC).

Mafunzo hayo ni matokeo ya makubaliano yaliyofikiwa na GGML na NEEC Julai 20 mwaka huu, kuhusu namna bora ya kuwasaidia wajasiriamali mkoani Geita ili wapate fursa bora ya kufanya biashara na taasisi mbalimbali nchini ikiwemo GGML.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa mafunzo hayo katika ukumbi wa kituo cha uwekezaji mjini Geita, Mkurugenzi Mtendaji wa GGML, Richard Jordinson alisema kampuni hiyo inalenga kuboresha ushiriki wa wafanyabiashara mkoani humo katika zabuni mbalimbali zinazotangazwa na kampuni hiyo.

Alisema malengo hayo ni kuwajengea uwezo ili wafahamu vigezo muhimu na kutimiza matakwa ya kisheria kusambaza bidhaa na huduma mbalimbali kwenye sekta ya uchimbaji madini sanjari na sekta zingine.

Aliongeza kuwa mafunzo hayo ni uthibitisho tosha kuwa kampuni ya GGML inakusudia kuchochea maendeleo endelevu kwa jamii inayozunguka mgodi.

“Tumeendelea kuthibitisha haya kwa vitendo kwa kushirikiana na Serikali kuboresha huduma za kijamii ikiwemo elimu, afya, maji, miundombinu ya barabara pamoja na shughuli mbalimbali za kuwawezesha wananchi kiuchumi maeneo yanayozunguka mgodi,” alisema Jordinson.

Alisema mpango huo unaotumia bajeti ya shilingi bilioni 1.3 za Kitanzania, unawalenga wajasiriamali 500 wanaoishi mkoani Geita wakiwemo vijana, wanawake na watu wenye ulemavu.

“Kufuatia mabadiliko ya Sheria ya Madini ya mwaka 2017, GGML kupitia fedha za Uwajibikaji wa Kampuni kwa Jamii imeshirikiana vyema na halmashauri mkoani Geita kutekeleza miradi ya maendeleo kwa jamii yenye thamani ya jumla ya shilingi za kitanzania bilioni 30 mkoani Geita,” alisema Jordinson.

Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC), Beng’i Issa aliipongeza GGML kwa mpango huo ambao unaendana na mpango wa kuendeleza biashara mkoani humo.

“Mpango huu utawajengea uwezo na kujiamini wajasiriamali na kushindana vyema na wafanyabiashara wengine nchini ili baadaye waweze kuboresha mapato na maisha yao,” alisema Beng’i Issa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles