24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

FFU jela miaka 30 kwa kubaka mwanafunzi

PICHA YA AKARI FFU ALIYEBAKA

NA ELIYA MBONEA, ARUSHA

ALIYEKUWA askari Polisi wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) mjini hapa, Raphael Makongojo, amehukumiwa kifungo cha miaka 30 jela, baada ya kukutwa na hatia ya kumbaka mwanafunzi.

Mbali na kifungo hicho, hukumu imemtaka kufanya kazi ngumu ikiwamo kupokea adhabu ya viboko 12 na kumlipa fidia ya Sh milioni 15 mwathirika wa tukio hilo.

Mama mzazi wa mwanafunzi huyo aliyebakwa pamoja na shangazi yake hawakuweza kusikiliza hukumu hiyo iliyosomwa faragha jana katika Mahakama ya Wilaya ya Arumeru baada ya kuzuiliwa kuingia ndani na askari magereza.

Akizungumza nje ya mahakama baada ya kusomwa kwa hukumu hiyo, mama mzazi wa mwanafunzi huyo, Hadija Ramadhani, alionyesha kufurahishwa na adhabu hiyo, huku akiiomba Serikali iongeze adhabu zaidi kwa wabakaji.

“Ni kweli nimejulishwa askari aliyembaka mwanangu amehukumiwa kifungo cha miaka 30 jela na adhabu nyingine. Naipongeza mahakama na Hakimu Jasmin Abdul kwa kutenda haki, Mungu ambariki.

“Ningeshauri makosa kama haya adhabu yake iwe kubwa zaidi, ikiwezekana kifungo cha maisha jela ili mhalifu wa aina hii asitoke nje kuchanganyikana na jamii tena,” alisema.

Mama huyo anayeishi mkoani Mwanza, alisema kwa ujumla kitendo hicho kimewaathiri kisaikolojia wanafamilia pamoja na binti yao, japokuwa wanaendelea kumwomba Mungu ili azidi kuwapa usahaulifu.

Baada ya hukumu hiyo, Makongojo alitolewa kwa ulinzi mkali wa askari magereza waliokuwa wamemfunga pingu, huku baadhi yao wakiwa na silaha za moto.

Makongojo alifikishwa mahakamani hapo na kusomewa mashtaka na Wakili wa Serikali, Sabina Silayo, aliyedai kuwa alitenda kosa hilo Januari 16, mwaka huu eneo la Kwa Mrombo jijini hapa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles