24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

DK SHEIN: HAKUNA RAIS MWINGINE Z’BAR

Na Muhammed Khamis (UoI)


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amevunja ukimya na kusema kuwa hakuna Rais mwingine wa Visiwa hivyo ila ni yeye ambaye anatambuliwa kwa mujibu wa Katiba.

Amesema hatamzuia aliyekuwa mgombeas urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 kupitia Chama cha CUF, Maalim Seif Sharif Hamad kuzungumza, akisema  licha ya kueneza propaganda za kufanyika mabadiliko ya uongozi hakuna lolote litakalofanyika hadi mwaka 2020.

Kauli hiyo aliitoa   mjini Unguja jana alipozungumza na waandishi wa habari kuhusu  mwaka mmoja tangu alipoingia madarakani Machi mwaka jana.

Dk. Shein alisema  licha ya baadhi ya wanasiasa kueneza kila aina ya maneno mitaani visiwani humo kuhusu mabadiliko katika uongozi  hakuna mabadiliko yoyote yatakayofanyika.

Alisema ni kawaida na hata Katiba ya nchi inatambua uhuru wa mtu kuzungumza kile anachokipenda ili mradi tu asivunje sheria za nchi.

Hata hivyo, alisema    wapo wanasiasa wamekuwa wakitumia kifungu hicho kuzusha maneno ya propaganda mitaani.

“Sitaweza kumzuia Maalim Seif  (Katibu Mkuu wa CUF), wala mwingine asiseme jambo lake maana anayo haki ya kufanya hivyo.

“Lakini nataka niwahakikishie tu kuwa Zanzibar hakutakuwa na mabadiliko ya uongozi wala uchaguzi mwingine hadi mwaka 2020,” alisema Dk. Shein.

Alisema hakuna asiyejua kuwa yeye ndiye rais wa Zanzibar   kwa mujibu wa Katiba na mamlaka inayoweza kumthibitisha ni Tume ya Uchaguzi pekee na si mtu mwingine yoyote.

Akizungumzia   mwaka mmoja  wa uongozi wake,  Rais Dk. Shein,  alisema Serikali imepiga hatua kubwa ya maendeleo   tangu ulipomalizika Uchaguzi Mkuu  Machi mwaka jana.

“Kuwapo amani na utulivu visiwani hapa ni miongoni mwa sababu kubwa zinazoifanya Serikali kukusanya kodi  kwa kiwango kikubwa zaidi ikilinganishwa na miaka ya iliyopita,” alisema.

Aliwataka wananchi wa Zanzibar kujikita zaidi katika kufanya kazi kwa sababu  ndiyo silaha ya kujikwamua katika uchumi badala ya kupiga maneno yasiyokuwa na tija.

Akieleza kuhusu mikakati mipya ambayo Serikali imedhamiria kuitimiza, alisema ni pamoja na kuhakikisha ina wataalamu wa kutosha ambao watakuwa wazalendo wa visiwa hivyo  kuepusha changamoto za aina tofauti ambazo zimeonekana kujitokeza kwenye  baadhi ya wizara kwa watendaji wake.

  Dk. Shein  alisema anasikitishwa na vitendo vilivyokithiri vya udhalilishaji wanawake na ubakaji wa watoto, vitendo ambavyo  Serikali haiwezi kuvifumbia macho.

 ‘’Katika kuhakikisha tunapambana na hali hii kwa sasa tumezuia   dhamana kwa wale wote ambao watakutwa na tuhuma za ubakaji mpaka   kesi zao zitakapoamuliwa na Mahakama,” alisema. 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles