24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Chadema watofautiana tena na polisi madai ya Mbowe kushambuliwa

MWANDISHI WETU -DAR ES SALAAM

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimesema hakina imani na uchunguzi unaofanywa na jeshi la polisi kuhusiana na tukio la Mwenyekiti wake, Freeman Mbowe.

Kimedai shambulizi la Mbowe linashabihiana na alilofanyiwa Makamu Mwenyekiti Bara, Tundu Lissu, na kwamba tofauti ni kiwango cha madhara.

Hivi karibuni Jeshi la Polisi kupitia kwa msemaji wake, David Misime, lilitoa ripoti inayoonyesha kuwa Mbowe hakushambuliwa kama inavyodaiwa bali alianguka kutokana na kulewa.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika, alisema chama kinaendelea kutafakari hatua za ziada za kuchukua.

Aliutaka umma upuuze njama alizodai zinatumika kuhalalisha kauli za uongo zinazotolewa katika kipindi hiki cha uchaguzi ili kuwachafua viongozi wa chama hicho na chama kwa ujumla.

“Tulidhani polisi itaendesha uchunguzi huu kitaalamu, kauli ya IGP (Mkuu wa Polisi, Simon Sirro) inaashiria bado jeshi linajihusisha katika propaganda hasi.

“Tuna vyanzo mbalimbali na mimi nimepata bahati ya kuzungumza na ambaye alikuwepo kwenye eneo la tukio, waliokwenda hospitali, maelezo ya wote hao hayaonyeshi popote kwamba mwenyekiti Mbowe alilewa chakari, nani aliyethibitisha, ajitokeze hadharani.

“Kipimo cha ulevi ni suala la kitabibu, ajitokeze daktari aiyempokea Mbowe na kumpima na polisi itoe ushahidi wa ‘CCTV camera’ kuthibitisha madai kwamba alianguka akiwa amelewa,” alisema Mnyika.

Alisema baada ya tukio hilo kutokea walifanya utaratibu wa kumleta Mbowe Dar es Salaam ili afanyiwe uchunguzi wa kitabibu kwenye maeneo mbalimbali ya mwili yakiwemo unyayo wa mguu na mguu wote kwa upana wake.

“Wakachukua X- ray ya sehemu ya kipande cha mguu ambacho hakikuvunjika wakaacha X- ray ambayo inaonyesha sehemu aliyopata madhara yaliyosababisha hadi afanyiwe operesheni ili kuhalalisha uongo kwamba hakuumia.

“Kiongozi wa kambi rasmi ya upinzani ana walinzi wa Serikali lakini tarehe 9 wameonekana nyumbani kwa Mbowe wakifanya mahojiano, je wamepata maelezo kwanini waliondolewa, na ikawaje baada ya kushambuliwa ndiyo wakarejesheshwa siku ya tarehe 9? Jeshi la polisi litoe maelezo,” alisema.

KUREJEA LISSU

Kuhusu suala la kurejea kwa Makamu Mwenyekiti wa Chadema Bara, Tundu Lissu, alilitaka jeshi la polisi liwahakikishie ulinzi wake pindi atakaporejea.

Kwa mujibu wa Mnyika, kwa nyakati kadhaa chama hicho kiliamuandikia barua IGP likimuomba ulinzi kwa ajili ya Lissu pindi atakaporejea lakini hazijajibiwa.

“Licha ya kukuandikia ujumbe Januari 7 mwaka huu bado hujatupatia majibu, kimya chako hiki hakipendezi, jaribio la mauaji dhidi ya Lissu lilizua maswali mengi sana ambayo hadi leo hayajapatiwa majibu…anaomba kupata ulinzi wakati atakaporejea nyumbani iweje leo linapata kigugumizi kutoa jibu la ombi hilo”? alihoji Mnyika.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles