23.3 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Afya ya sitta utata

samuel-sittaNa Mwandishi Wetu-DAR ES SALAAM

HALI ya afya ya Spika mstaafu wa Bunge la tisa, Samuel Sitta, imezidi kuwa siri nzito baada ya kurudishwa nchini kimya kimya kutoka  Ujerumani alikokuwa amepelekwa  kwa matibabu.

Habari za uhakika ambazo MTANANIA ilizipita  Dar es Salaam jana, zinaeleza kuwa Sitta alirudishwa nchini mwishoni mwa wiki iliyopita ingawa taarifa zake zimezidi kuwa siri.

Kiongozi huyo aliyejizolea sifa lukuki wakati wa Bunge la tisa, hajaonekana hadharani kwa muda mrefu tangu ulipomalizika mchakato wa kumpata Spika wa Bunge la 11 mwaka jana.

Septemba 28, mwaka huu, gazeti hili lilipoti taarifa za Sitta kupelekwa Ujerumani kwa matibabu, taarifa  zikisema amekuwa akisumbuliwa zaidi na miguu.

Kiongozi mmoja wa Serikali aliiambia MTANZANIA jana kuwa Sitta alirudishwa nchini wiki iliyopita baada ya kupata ushauri wa kina wa jopo la madaktari.

“Ni kweli mzee wetu Sitta amerudishwa nyumbani kutoka Ujerumani ambako alipelekwa kwa matibabu zaidi.

“Sijajua vizuri sababu ya kurudishwa kwa vile alipelekwa mgonjwa, nadhani suala hili linaweza kuzunguzwa vizuri na familia yake ambayo iko karibu zaidi.

“Nakumbuka hata kabla hajapelekwa Ujerumani alitembelewa na viongozi wetu wa taifa mbalimbali ambao naamini walimshauri akapate tiba nje.

“Lakini siku zote madaktari wanajua hali ya mgonjwa…kubwa ambalo naliomba ni kwamba Mungu amsaidie arudi katika hali yake  ya kawaida,”alisema kiongozi huyo.

Taarifa zinasema kabla ya kupelekwa Ujerumani, hali yake ilibadilika ghafla.

MTANZANIA pia ilimtafuta mke w wa Sitta, Margaret,  kuhusu hali ya mume wake lakini alijibu kwa kifupi kuwa:

“Baba nakuomba sana uwe na subira nina kikao cha familia, nitafute baadaye”.

Wakati mke wa Sitta akisema hayo,  mtoto wa mwanasiasa huyo ambaye pia ni mbunge wa zamani wa Urambo Magharibi, Benjamin, alisema hali ya baba yake inaendelea vizuri na wanamshukuru Mungu.

“Tunamshukuru Mungu hali ya baba inaendelea vizuri, amerudi kutoka Ujerumani,” alisema Benjamin ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Msasani kupitia CCM.

Septemba 19, mwaka huu, Rais Dk. John Magufuli alimtembelea Sitta hospitalini alikokuwa amelazwa ili kumjulia hali kisha akamwombea dua Mungu amsaidie.

Siku iliyofuata, Waziri Mkuu,  Kassim Majaliwa naye alimtembelea hospitalini kumjulia hali.

Sitta ameshika nyadhifa mbalimbali serikali ikiwamo  Uspika wa Bunge kuanzia mwaka 2005 hadi 2010, uwaziri na ubunge kwa kipindi kirefu.

Pia alikuwa Mwenyekiti wa Bunge la Katiba na pia alikuwa  miongoni mwa wanachama zaidi ya 40 wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) waliochukua fomu za kugombea urais mwaka jana.

Hata hivyo, baada ya Kamati Kuu ya chama hicho kumuondoa katika kinyang’anyiro hicho, alitangaza kustaafu rasmi siasa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles