23.6 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

YANGA MKUBALI KUJIJENGA UPYA

NA ZAINAB IDDY


NI ukweli uliowazi hivi sasa mabingwa wa watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara ‘Yanga’,  wanaonekana kutoka katika ushindani, tofauti na misimu mitatu iliyopita jambo linalowatia shaka mashabiki wake wengi, huku wakijiuliza iwapo kama timu yao itaweza kutetea taji lake.

Mwanzoni mwa msimu kila mwanayanga alijijengea imani kuwa ni lazima timu hiyo ichukue ubingwa kwa mara ya nne mfululizo, lakini sasa jambo hilo linaonekana kuwa ndoto, kulingana na mwenendo wa matokeo kusuasua.

Yanga iliyokuwa tishio ndani na nje ya uwanja, leo hii inakubali kufungwa au kutoka sare na timu ndogo kama Mwadui FC, Mbao FC, Ndanda FC na nyinginezo ambazo awali ilikuwa ikikutana nazo, inavuna pointi tatu.

Ingawa mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu Tanzania Bara haujakamilika, lakini kwenye mechi 13 walizocheza timu hiyo chini ya kocha Geogre Lwandamina, imeonekana kutokuwa na morari ya kucheza soka la ushindani wengi wakipenda kuliita la kampa kampa tena.

Tukirejea misimu miwili iliyopita, klabu hiyo kongwe nchini ilitawaliwa na idadi kubwa ya wachezaji wenye uwezo wa kupambana na kupata matokeo chanya katika uwanja wowote, pasipo kuangalia timu gani wanacheza nayo jambo ambalo msimu huu halipo.

Unaweza kujiuliza sababu ya Yanga kuwa katika hali hii ni nini ?, bila ya chembe cha unafki hata kidogo Kiroho safi  hivi sasa ukweli ni kuwa timu hiyo inakabiliwa na matatizo lukuki ya ndani ya uwanja kwa maana ya kiufundi, kiutawala na kiuchumi.

Unaweza kushangaa kiufundi kivipi, wakati wachezaji wao waliokuwa wakiwapa matokeo bado wapo, jibu ni jepesi sana hivi sasa wale unaowaona ndio jicho kwenye timu, ambapo wengine  wamekuwa wakichoma mahindi na kula mishahara ya bure, ambapo wameonekana kutokuwa na msaada na sababu kubwa ikiwa ni majeraha, lakini pia kupoteza morari ya kuitumikia timu hiyo, baada ya kutolipwa mishahara yao kwa wakati.

Hivi sasa Yanga iliyokuwa ikiweka kambi  Uturuki, inakaa miezi minne bila ya kuwalipa mishahara wachezaji, leo hii inashindwa kuwalipa fedha za usajili wachezaji wao na hata kuingia kwenye mfumo wa kusajili wachezaji wa mafungu kweli kila zama zinawakati wake.

Bila ya kificho Yanga ina hali mbaya na hata kama atakuja bilionea kuwekeza, bado hawatoweza kumaliza madeni wanayodaiwa, kitu ambacho uongozi unalazimika kuwalipa wachezaji kwa mafungu tena wale wanaoonekana kupiga kelele hadaharani, huku wenzangu na mie wasioweza kufungua midomo wakiwa wanaendelea kuhesabu miezi na kuweka mgomo baridi uwanjani kwa kucheza chini ya kiwango au kila kukicha, wakidai wana majeraha hata kama hawana.

Kwa hali iliyopo hivi sasa ni ngumu Yanga kutetea taji lake ikiwa na matatizo lukuki ya kiufundi, kiuchumi na kiutawala,  hivyo si vibaya kukubalia tu kujijenga upya.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles