23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Wanafunzi Chuo cha KIU watua kwa DC

NA GRACE SHITUNDU, DAR ES SALAAM
WANAFUNZI wa Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Kampala (KIU) kilichopo Gongolamboto jana waliwasilisha malalalamiko yao kwa Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Raymond Mushi baada ya kufanya mgomo kwa vipindi tofauti bila kupata majibu.
Mamia ya wanafunzi hao walifika katika ofisi ya mkuu wa mkoa saa 6 mchana kwa lengo la kupeleka kilio chao kwa Mkuu wa wa Mkoa wa Dar es Salaam, Meck Sadik hata hivyo waligonga mwamba kwa kushindwa kuonana naye.
Baada ya kukosekana kwa Sadik, ilimlazimu DC Mushi, kutoka ofisi kwake na kwenda kusikiliza kilio cha wanafunzi hao.
Akizungumza kwa niaba ya wenzake, mwanafunzi wa mwaka wa kwanza anayechukua Shahada ya Sayansi katika chuo hicho, Jackson Raymond, alisema kuwa wanafunzi hao wana hoja takribani 15 katika mkutano huo baina yao na mkuu huyo wa wilaya.
Alisema wanafunzi waliomaliza kozi mbalimbali katika chuo hicho wamekua hawatambuliki pindi wanaopoomba ajira baada ya kumaliza masomo yao kwa madai kuwa chuo hakitambuliki kwa kuwa hakina usajili.
“Kuna baadhi ya wenzetu wamemaliza chuo lakini wakienda kuomba ajira wanaambiwa chuo walichosoma hakitambuliki kwa kuwa hakijasajiliwa, hivyo tunataka kujua na sisi hatima yetu itakuaje baada ya kumaliza masomo.
“Na hata tukiuliza endapo tutamaliza masomo tutapata vyeti vya wapi maana chuo hakijasajiliwa nchini tunaambiwa vitatoka makao makuu Kampala, Uganda” alisema Jackson.
Alisema licha ya wasiwasi wa usajili, lakini uongozi wa chuo hicho umeweka ada kubwa ambayo tayari Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ilitoa barua Novemba 13, mwaka jana kuwataka wapunguze lakini suala hilo halijafanyika hadi sasa.
Alisema matatizo mengine ni pamoja na mitaala inayotumika haijulikani kuwa ni ya nchi gani Tanzania au Uganda, kwani kumekuwa na masomo mengi pamoja na utaratibu mbaya wa utoaji wa mitihani na matokeo.
Baada ya kusikiliza malalamikio yao DC Mushi, aliwatuliza wanafunzi hao huku akiwataka wampe muda ili aweze kufutilia suala hilo kwa mamlaka zinazohusika.
“Nimesikiliza maelezo yenu na nimegundua kuwa kuna matatizo katika utendaji kwani Nacte na TCU walifanya kazi yao na hivyo Bodi ya Mafamasia wameomba niwape siku tano na mimi nawaambia mpaka Jumatatu nitakukuwa nimeshapata majibu ya kudumu ya matatizo yenu,” alisema.
Septemba, mwaka jana wanafunzi hao wa KIU, walikwenda Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kwa lengo la kumwona Waziri, Dk. Shukuru Kawambwa, lakini hawakufanikiwa kumwona.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles